Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 14 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 111 2018-04-20

Name

Twahir Awesu Mohammed

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mkoani

Primary Question

MHE. TWAHIR AWESU MOHAMED aliuliza:-
Jeshi la Polisi lina dhamana kubwa ya kulinda usalama wa raia na mali zao na ni msimamizi mkuu katika haki za binadamu:-
(a) Je, ni lini Jeshi hilo litafanya kazi zake kisayansi zaidi na kuondokana na kutumia nguvu zisizo za lazima wakati wa kutekeleza majukumu yake?
(b) Je, suala la weledi kwa watendaji wa polisi linasimamiwa vipi ili polisi waweze kupambana na uhalifu unaokua kitalaam kila siku?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Twahir Awesu Mohamed, Mbunge wa Mkoani lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi ni chombo kilichoanzishwa kwa mujibu wa Katiba kusimamia usalama wa raia na mali zao na katika utendaji wake linaongozwa na sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali. Aidha, Jeshi la Polisi limejiwekea kanuni za kudumu (PGO) ambazo zimetafsiri na kutoa mwongozo wa utekelezaji wa sheria zote zinazoongoza utendaji wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa kazi zake askari anaruhusiwa kutumia nguvu inayoendana na mazingira ya tukio. Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kifungu namba 11(2) kinamruhusu askari kutumia nguvu katika ukamataji iwapo mkamatwaji atakaidi. Pia PGO 274 inaeleza mazingira ya matumizi ya nguvu na aina ya nguvu inayopaswa kutumika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikiwajengea uwezo wa kiutendaji askari kwa kutoa mafunzo mbalimbali sehemu za kazi yenye lengo la kuwakumbusha taratibu za kazi, pia limekuwa likitoa mafunzo ya weledi ya ndani na nje ya nchi ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha linafanya kazi zake kwa weledi Jeshi la Polisi limekuwa likiajiri wasomi wenye taaluma mbalimbali kama vile TEHAMA, maabara, uchunguzi wa nyaraka na taaluma zingine zinazohusiana na makosa yanayosababishwa na ukuaji wa teknolojia.