Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 12 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 98 2018-04-18

Name

Richard Phillip Mbogo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nsimbo

Primary Question

MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Serikali imeendelea na juhudi mbalimbali za kulinda Nyara za Serikali:-
Je, vitalu vya uwindaji vinachangia kiasi gani katika upotevu wa Nyara za Serikali?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, uwindaji wa kitalii ni sehemu ya matumizi endelevu ya wanyamapori na unafanyika kwa mujibu wa Sera ya Wanyamapori ya Mwaka 2007, Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori, Sura 283 na Kanuni za Uwindaji wa Kitalii za Mwaka 2015 zikisomwa kwa pamoja, pamoja na marekebisho yake ya mwaka 2017. Ili uwindaji uweze kufanyika, kampuni iliyopewa kitalu huomba na kupatiwa mgao wa wanyamapori (quota) watakaowindwa katika msimu husika. Mgao wa wanyamapori huandaliwa na Kamati ya Ushauri wa Mgao wa Wanyamapori (Quota Allocation Advisory Committee).
Mheshimiwa Mwenyekiti, vigezo vinavyotumika kutoa mgao ni pamoja na; moja, idadi ya wanyamapori (population status) kulingana na sensa; pili, taarifa kutoka kwa Maafisa Wanyamapori wa maeneo yanayohusika; tatu, mafanikio katika matumizi ya mgao wa wanyamapori (offtake levels); nne, ukubwa wa nyara zinazopatikana mwaka hadi mwaka (trend of trophy size) na tano, matakwa ya Mikataba ya Kimataifa kama vile CITEs.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imeweka udhibiti wa kutosha ili kuzuia uwezekano wa kupotea nyara wakati wa uwindaji. Udhibiti huo unaanzia kwenye kutoa vibali ambavyo ni vya kielektroniki, usimamizi porini wakati wa uwindaji ili kuhakikisha aina na idadi ya wanyamapori wanaowindwa waliotolewa kwenye kibali inazingatiwa, umilikishwaji wa nyara zilizowindwa na ukaguzi wa nyara kabla ya kusafirishwa kwenda nje ya nchi. Aidha, pale inapotokea ukiukwaji wa sheria na kanuni wahusika hufikishwa mbele ya sheria na adhabu stahiki hutolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu imeendelea kuongeza udhibiti katika usimamizi wa uwindaji wa kitalii kwa kutumia sheria na kanuni ambazo wanyamapori huwindwa kwa kuzingatia jinsi, umri na ukubwa wa nyara. Udhibiti huo umesaidia kupunguza uwezekano wa wanyamapori kupungua kutokana na kuwindwa na pia kumesaidia kupatikana kwa mapato yatokanayo na uwindaji wa kitalii. Hivyo basi, vitalu vya uwindaji husaidia katika kulinda na kuhifadhi nyara na kutoa mchango katika uchumi wa nchi, hasa kwa kuchangia fedha za kigeni, kutoa ajira kwa wananchi na kuchangia maendeleo ya jamii.