Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 8 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 64 2018-04-12

Name

Josephine Johnson Genzabuke

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:-
Zahanati nyingi za Vijiji vya Mkoa wa Kigoma katika wilaya zote zina upungufu mkubwa sana wa watumishi wa afya na baadhi ya zahanati hazina Waganga hivyo huduma zinatolewa na Manesi Wasaidizi tu:-
Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi wa afya wa kutosha katika maeneo hayo ili kuimarisha utoaji wa huduma za afya vijijini?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kigoma una jumla ya vituo vya kutolea huduma za afya 278, hospitali sita (6), vituo vya afya 32 na zahanati 240. Kati ya vituo hivyo, vituo vya Serikali ni 224 sawa na asilimia 80%, hospitali tatu (3), vituo vya afya 23 na zahanati 198. Idadi hii inajumuisha vituo vya mashirika ya dini, kambi za wakimbizi, binafsi na taasisi za umma kama Magereza, Polisi, Jeshi na TRL.
Mheshimiwa Spika, mahitaji ya watumishi wa sekta ya afya kwa mujibu wa ikama mpya ya mwaka 2014 katika vituo vya umma kimkoa ni 5,007, watumishi waliopo ni 1,663 sawa na asilimia 33.2 ya mahitaji na upungufu ni 3,344 sawa na asilimia 66.8. Mkoa pamoja na halmashauri zimeendelea kukabiliana na changamoto hii kwa kushawishi wadau wa sekta ya afya wakiwemo THTS, East African Public Health Lab Net, Engender Health na UNICEF kusaidia kuajiri watumishi muhimu kwa muda/mkataba, pamoja na kuweka katika bajeti kwa ajili ya kuajiri watumishi wapya.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2017/ 2018, Mkoa wa Kigoma umepatiwa watumishi wa afya 95 wakiwemo Madaktari watano (5), Matabibu 24, Wauguzi 33, Wafamasia 17 na Wataalam wa Maabara 16. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, mkoa umeomba kutengewa nafasi za ajira 1,667 kwa kada mbalimbali za afya.