Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 4 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 24 2018-04-06

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-
Je, ni lini ujenzi unaoendelea katika Vituo vya Afya Ikuti, Wilayani Rungwe na Ipinda Wilayani Kyela utakamilika ili kuwawezesha wananchi wa maeneo hayo kupata huduma kwa wakati?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya cha Ikuti kimekarabatiwa katika awamu ya kwanza ya ukarabati wa vituo vya afya 44 ulioanza tarehe 10 Oktoba, 2017 na kukamilika tarehe 31 Januari, 2018 kwa gharama ya shilingi milioni 500 ili kuongeza huduma za upasuaji wa dharura kwa mama wajawazito. Aidha, shilingi milioni 220 zimetolewa kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba vya upasuaji na samani. Kituo hicho kinaendelea kutoa huduma zote za matibabu isipokuwa huduma za upasuaji wa dharura. Ujenzi wa majengo ya Kituo cha Afya Ikuti umekamilika na kinachosubiriwa kwa sasa ni vifaatiba kutoka Bohari ya Dawa (MSD).
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa kituo cha afya cha Ipinda ulianza Oktoba, 2017 katika ujenzi huu jumla ya majengo mapya nane yamejengwa pamoja na ukarabati wa jengo la wagonjwa wa nje, uwekaji wa miundombinu ya maji safi na majitaka, kichomea taka na ujenzi wa njia zinazounganisha majengo (walk way). Jumla ya shilingi 625,899,806 zimetumika mpaka sasa katika mchanganuo ufuatao; Serikali Kuu shilingi 500,000,000, Halmashauri pamoja na wadau shilingi 90,100,975.40 na wananchi 35,798,830.60.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majengo hayo, Halmashauri ya Wilaya ya Kyela imepokea vifaatiba kutoka MSD vyenye thamani ya jumla ya shilingi 73,909,900 na vilivyosalia vinatarajiwa kupatikana mnamo mwezi huu wa nne. Vilevile Halmashauri imenunua vitanda 47, magodoro na mashuka vyenye thamani ya shilingi 27,066,500 ambavyo vimefungwa na vinatumika katika majengo hayo. Kituo cha Afya Ipinda kinaendelea na ujenzi wa miundombinu kwa gharama ya shilingi milioni 500 ambao unahusisha kupanua huduma za upasuaji wa dharura na shilingi milioni 220 zimetolewa kwa ajili ya vifaatiba vya upasuaji na samani. (Makofi)