Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 57 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 475 2017-06-30

Name

Dr. Mary Machuche Mwanjelwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mbeya Mjini

Primary Question

MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA aliuliza:-
Je, nini sera ya Serikali katika kubadilisha mandhari ya maeneo ambayo ni squatter au ya wazi kwa kuwekeza katika majengo ili kuwa na makazi ya kisasa kwa ajili ya wananchi kwa kutumia ardhi iliyopo katika eneo husika?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali namba 475 la Dkt. Mary Mwanjelwa, Mbunge wa Viti Maalumu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kifungu namba 4.1.4.2 cha Sera ya Taifa ya Makazi ya mwaka 2000 kinaelekeza kuwa maeneo yaliyojengwa bila kupangwa na kuwekewa huduma za msingi yaboreshwe na wananchi wenyewe kwa kushirikiana na asasi za kijamii. Kwa maeneo yaliyojengwa bila kupangwa na kupimwa lakini yapo katikati ya miji (prime areas) hususan katika Jiji la Dar es Salaam, Wizara imeandaa rasimu ya mkakati wa uboreshaji wa maeneo hayo kwa kutumia dhana ya kukusanya ardhi (land pooling). Utekelezaji wa dhana hii utawawezesha wananchi wa maeneo husika kupata makazi bora na pia kupata ardhi kwa ajili ya uwekezaji mpya.
Mheshimiwa Spika, dhana ya kukusanya ardhi inalenga kuboresha maeneo hayo kwa kujenga majengo makubwa ya ghorofa ili kuweza kuwapatia makazi mbadala wakazi wa maeneo husika katika eneo hilo hilo, na pia kupata eneo la uwekezaji utakaojumuisha ujenzi wa majengo ya kibiashara kama vile maduka makubwa (super markets and shopping malls), makazi ya maghorofa ambayo mengi yanakuwa na apartments, hoteli, huduma za kijamii, maeneo ya wazi, maeneo ya burudani na kadhalika.
Mheshimiwa Spika, rasimu hiyo kwa awamu ya kwanza inapendekeza kufanya ukusanyaji wa ardhi katika maeneo ya Manzese, Vingunguti, Buguruni, Msasani, Keko, Namanga, Mikocheni na Kawe.