Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 57 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 469 2017-06-30

Name

Rose Kamili Sukum

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ROSE K. SUKUM aliuliza:-
Serikali ina utaratibu wa kutoa fedha kwa ajili ya shule za bweni nchini. Kwa kipindi cha kuanzia tarehe 31/08/2013 hadi 10/02/2014 Halmashauri ya Hanang ilipokea kutoka Serikali Kuu kiasi cha shilingi 508,779,500 kwa ajili ya chakula cha shule za bweni. Taarifa zinaonesha kuwa fedha zilizotumika kununua chakula ni shilingi 225,585,000. Kwa takwimu hizo bakaa ni shilingi 283,194,500 na kwa mujibu wa mkaguzi, bakaa hiyo haionekani kwenye akaunti yoyote ya benki.
(a) Je, fedha hizo zinarudishwa Hazina bila ya uwepo wa nyaraka zozote toka Halmashauri kuonesha muamala unavyofanya kazi?
(b) Je, kama fedha hizo hazikurudishwa Hazina, nani anaweza kuidhinisha matumizi bila ya mpango wake kupitishwa na Kamati ya Fedha na Mipango ya Halmashauri?
(c) Je, kama fedha zimetumika bila kupangiwa na Kamati halali, ni kwa nini wahusika bado wanaendelea kuwa ofisini bila ya kufunguliwa mashtaka ya wizi wa kuaminika?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA SERIKALI ZA MITAA: alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose Kamil Sukum, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ ilipokea kiasi cha fedha shilingi 508,779,500 kwa ajili ya chakula cha shule za msingi nne za bweni ambazo ni Katesh, Balangdalalu, Bassodesh na Gendabi. Jumla ya shilingi milioni 225.58 zilizopangwa kwenye bajeti zilipelekwa kwenye shule za msingi za bweni kadiri fedha hivyo zilivyopokelewa kutoka Hazina. Kiasi cha shilingi milioni 283.19 zilizosalia hazikurudishwa Hazina badala yake fedha hizo zilibadilishiwa matumizi kwa kuombewa kibali cha kubadilisha matumizi kwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango kwa barua yenye kumb. Na. HANDC/ED/F.1/12/ VOL.IV/198 ya tarehe 10/04/2014 na kwa Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kwa barua yenye kumb. Na. HAN/ED/F1/12/ VOL.IV/205 ya tarehe 01/08/2014.
Mheshimiwa Spika, Kamati ya Fedha na Mipango ya Halmashauri baada ya kupokea taarifa ya matumizi ya fedha, iliagiza fedha hizo zirudishwe kupitia mapato ya ndani kwa ajili ya kutekeleza shughuli za ununuzi wa vifaa na samani kwa wanafunzi wa shule husika. Ili kutekeleza agizo hilo, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2015/2016, kiasi cha shilingi 130,000,000 zilipelekwa kwenye akaunti za vijiji vya Gendabi, Bassodesh, Katesh na Balangdalalu kwa ajili ya kununulia magodoro, vitanda na ukarabati wa mabweni kwa shule za msingi za bweni zilizopo kwenye vijiji hivyo. Aidha, Halmashauri imeagizwa kurejesha fedha zilizobaki kiasi cha shilingi milioni 153.19 ndani ya mwaka huu wa fedha.
Mheshimiwa Spika, kutokana na matumizi ya fedha za halmashauri yasiyoridhisha, ikiwa ni pamoja na matumizi ya fedha hizo, tangu mwezi Aprili, 2016, Mkurugenzi Mtendaji amesimamishwa kazi na mamlaka yake ya nidhamu. Aidha, watumishi wengine wanne akiwemo afisa mipango wilaya, mweka hazina wilaya na wahasibu wawili wamesimamishwa kazi na Baraza la Madiwani ili kupisha uchunguzi.