Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 49 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 400 2017-06-16

Name

Cecilia Daniel Paresso

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CECILIA D. PARESSO aliuliza:-
Sheria ya Tawala za Mikoa Sura ya 97 inawapa mamlaka ya kipolisi Wakuu wa Mikoa na Wilaya kuwatia nguvuni watu wa muda wa saa 48, lakini sheria hiyo imekuwa ikitumiwa vibaya na Wakuu wa Mikoa na Wilaya kwa kutoa amri za kukamata Wabunge, Wenyeviti wa Halmashauri, Madiwani, Wenyeviti wa Vijiji, Mitaa na hata watumishi wa umma wakiwemo madaktari.
• Je, Serikali inawachukulia hatua gani Wakuu wa Mikoa na Wilaya wanaotumia vibaya madaraka na sheria hiyo?
• Je, ni lini Serikali itaifanyia marekebisho sheria hiyo ili kuwaondolea Wakuu wa Mikoa na Wilaya mamlaka ya kuwaweka watu ndani kwa kuwa ni kandamizi, inakiuka haki za binadamu na inatumika vibaya?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais –TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu
(a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakuu wa Mikoa na Wilaya kisheria ni wasimamizi wa shughuli zote za Serikali katika maeneo yao ya utawala. Hivyo, ni jukumu lao kuchukua hatua pale sheria za nchi zinapokiukwa ili kuhakikisha kunakuwepo amani na usalama kwa ustawi wa wananchi na Taifa kwa jumla. Hata hivyo, wapo baadhi ya Wakuu wa Mikoa na Wilaya ambao wanatumia vibaya mamlaka yao, tayari Serikali imetoa maelekezo mahususi kuzingatia mipaka yao ya kazi katika kutekeleza majukumu waliyokabidhiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia kuwa Wakuu wa Mkoa na Wilaya wamepewa madaraka ya kuwa mlinzi wa amani na usalama (peace and security). Kifungu cha 7 na 15 vya Sheria ya Tawala za Mikoa, Sura, 97 Vinawapa Mamlaka viongozi hao kumweka ndani mtu yeyote kwa muda wa saa 48 ikiwa itathibitika kuna hatari ya uvunjifu wa amani na usalama au mtu huyo ametenda kosa la jinai. Tumetoa maelekezo yanayofafanua matumizi mazuri ya sheria hii kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya wote pamoja na mafunzo kuhusu mipaka na majukumu ya kazi zao, hivyo kwa sasa sheria inajitosheleza, ila tutaendelea kusisitiza matumizi sahihi ya sheria husika.