Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 10 2018-04-04

Name

Suzana Chogisasi Mgonukulima

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. GODFREY W. MGIMWA (K. n. y. MHE. SUZANA C. MGONOKULIMA) aliuliza:-
Tangu kutangazwa sheria ya kuzitaka Halmashauri zote nchini kutenga asilimia 10 ya mapato yake kwa ajili ya wanawake na vijana.
Je, ni nini kinaifanya Serikali kutokuwa na taarifa ya mfuko huo kujua una kiasi gani cha fedha?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Suzana Chogisasi Mgonokulima, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, chimbuko la maelekezo yanayozitaka Halmashauri zote nchini kutenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya mikopo ya wanawake asilimia tano na mikopo ya vijana asilimia tano ni Azimio la Bunge la Agosti 1993, chini ya kifungu cha 17(1) cha Sheria ya Exchequer and Audit Ordinance ya mwaka 1961; likiazimia kuanzishwa kwa Mifuko Maalum ya Mikopo kwa Vijana na Wanawake kwa kuchangiwa asilimia 10 ya mapato ya ndani ya kila halmashauri kila mwaka. Baada ya azimio hilo Serikali ilitoa maelekezo mahsusi kwa Halmashauri zote nchini kutenga fedha hizo kuanzia mwaka wa fedha 1993/1994.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto kadhaa za kiutekelezaji ambazo zimekuwa zikisababisha utekelezaji wa azimio hilo usifikie asilimia 100. Miongoni mwa changamoto hizo ni kutofikia viwango vya makusanyo ya ndani vilivyopangwa kwa mwaka husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, mfano katika mwaka wa fedha 2016/2017 jumla ya shilingi 665,414,828,000 za mapato ya ndani zilipangwa kukusanywa na Halmashauri zote nchini; lakini mapato halisi yaliyokusanywa ilipofika mwisho wa mwaka yalikuwa ni shilingi 544,897,803,696 tu. Kutokana na ukusanyaji kutotabirika na hivyo kutofikia viwango tarajiwa, badala ya kiasi cha shilingi bilioni 56.8 kukopeshwa wanawake na vijana kama ilivyokuwa imetengwa, ni shilingi 17.5 tu sawa na asilimia 31, ndizo zilizotolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwakumbusha wakurugenzi wa halmashauri zote 185 Tanzania Bara kwamba kutotoa asilimia 10 ya mapato ya ndani ni tabia ambayo husababisha waandikiwe deni kwenye taarifa za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali. Kupitia Bunge lako Tukufu, naagiza kuanzia sasa ni lazima kila Halmashauri itoe asilimia 10 ya mapato halisi ya ndani kama ilivyoelekezwa na Serikali ili kutokusababisha madeni ya aina hiyo.