Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 8 Energy and Minerals Wizara ya Madini 103 2018-02-08

Name

Anna Joram Gidarya

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANNA J. GIDARYA aliuliza:-
Mgodi a Tanzanite ulioko Mererani, Wilaya ya Semanjiro ni mgodi wenye idadi kubwa ya vijana wanaofanya kazi katika mgodi huo na kumekuwa na historia ya matukio ya maafa kila mwaka ya vifo vya watu wengi.
(a) Je, Serikali imefanya utafiti gani ili kubaini chanzo cha maafa hayo yanayolikumba Taifa kila mwaka na kusababisha kupoteza nguvu kazi ya Taifa letu?
(b) Je, Serikali haioni umuhimu wa kuanzisha utaratibu maalum kwa wamiliki wa vitalu vya Tanzanite kuwalipa kifuta jasho wahanga wote wanaopatwa na maafa wanapokuwa kazini?

Name

Doto Mashaka Biteko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukombe

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. DOTO M. BITEKO) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anna Joram Gidarya, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, mapitio ya taarifa za ajali yanaonesha kuwa ajali nyingi husababishwa na wachimbaji wadogo kutokuzingatia tahadhari ya usalama wanapotekeleza majukumu yao ya uchimbaji madini. Hivyo, Serikali imekuwa ikifanya juhudi za ukaguzi wa maeneo ya uchimbaji na kuwaelimisha wachimbaji kuchukua tahadhari za usalama wakati wa kufanya kazi pamoja na kuwahamasisha kuunda timu za wakaguzi katika maeneo yao kutoka miongoni mwa wachimbaji ambao hupewa elimu ya ukaguzi na wataalam wetu wa Wizara ya Madini. Hivyo, nawasihi wachimbaji wa madini kutambua umuhimu wa kuzingatia taratibu na usalama wa kazi kwa uchimbaji ili kulinda afya na uhai wao.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali imeanzisha Mfuko wa Fidia ya Wafanyakazi kupitia Sheria Namba 20 ya mwaka 2008 ya Fidia ya Wafanyakazi. Wizara itahamasisha wamiliki wa leseni na wachimbaji kujiunga na mfuko huu ili kupata kifuta jasho wanapopatwa na maafa wanapokuwa kazini.