Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 6 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 71 2018-02-06

Name

Lucy Simon Magereli

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LUCY S. MAGERELI aliuliza:-
Matatizo ya migogoro ya ardhi na Mipango Miji ni suala nyeti sana linalohitaji kutazamwa sana katika zama hizi; na hivi karibuni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi aligawa ramani za maeneo ya mitaa ya Jiji la Dar es Salaam lakini zoezi hilo halikufanikiwa kutokana na kukosa mkakati ulioambatana na matumizi ya ramani hizo:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha ramani hizo zinapatikana kwa nchi nzima ili kusaidia kuongoza matumizi ya ardhi katika miji mingi nchini?
(b) Waziri Mkuu aliyepita Mheshimiwa Mizengo Pinda alisema Serikali ingeuza Government Bond ili kupata fedha za kugharamia mradi huo; Je, agizo hili limefikia hatua gani katika utekelezaji?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy Simon Magereli Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria Na. 8 ya Mipango Miji ya Mwaka 2007 katika Kifungu cha 21(1) inazipa Halmashauri mamlaka ya kupanga na kuhakikisha ramani za Mipango Miji ya jumla (master plan) na ile ya kina (michoro ya mipango miji) iliyoidhinishwa na Wizara yenye dhamana na ardhi zinahifadhiwa na kusambazwa kwa wadau. Halmashauri zinaendelea kutekeleza jukumu hili kwa kutoa elimu na tafsiri sahihi ya michoro ya Mipango Miji kwa wananchi ili kuhakikisha kunakuwa na usimamizi shirikishi kwa lengo la kudhibiti uendelezaji holela.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Serikali kuuza bond ili kupata fedha za kugharamia mradi huu, suala hili halijatekelezwa badala yake kila Halmashauri imeelekezwa kutumia vyanzo vyake vya mapato ya ndani kwa kushirikiana na sekta binafsi. Utaratibu huu unatokana na Sheria ya Mipango Miji inayotoa fursa kwa wamiliki binafsi wa ardhi kuandaa mipango ya matumizi kwa mujibu wa sheria.