Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 6 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 69 2018-02-06

Name

Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Primary Question

MHE. JASSON S. RWEIKIZA aliuliza:-
Maeneo mengi ya Bukoba Vijijini kama vile Kata za Ruhunga, Kibirizi, Izimbya, Mugajwale, Rukoma, Kikomelo na nyingine yana tabu kubwa sana ya upatikanaji wa maji na kilio hiki kimekuwa cha muda mrefu sana:- Je, ni kwa nini Serikali haichukui hatua ya kuwasaidia wananchi hao.

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jasson Samson Rweikiza, Mbunge wa Bukoba Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hali ya upatikanaji wa huduma za maji kwenye maeneo aliyoyataja bado ni changamoto. Hata hivyo, kwa uhalisia hali hiyo ni tofauti na maeneo mengi ya Halmashauri ya Bukoba Vijijini ambako Serikali imekamilisha hivi karibuni miradi 18 ya maji kwenye Kata za Nyakibimbili, miradi mitatu (3); Kyamulaile, miradi mitatu (3); Kemondo, miradi mitatu (3); Buteragunzi, miradi minne (4); Rubole, mradi mmoja (1); Karabagaine, mradi mmoja (1); Rubafu (mradi mmoja (1); na Mikoni, miradi miwili (2) iliyogharimu shilingi 3,552,117,690 inayohudumia wakazi 61,279; hali hiyo imeinua upatikanaji wa maji hadi kufikia asilimia 64 ya upatikanaji wa maji kwa wakazi wote wa Bukoba Vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya upatikanaji wa maji itapanda zaidi hadi kufikia asilimia 75 ifikapo mwezi Juni, 2018 kutokana na kukamilika kwa miradi ya Rukoma, Ubwera, Katoma na Kibirizi inayogharimu Sh.2,235,274,135 na itakayohudumia wakazi 18,449.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa kuna visima 75 vinavyofanya kazi kwenye Kata ya Rukoma, Ruhunga, Butulage, Mgajwale, Izimbya, Katoro, Rubale, Kaibanja, Kishogo, Kasharu, Maruku na Kikomero; na vyanzo vingine 90 vya maji kwenye Kata za Nyakato, Buhendagabo, Katerero na Bujugo. Serikali itatekeleza miradi ya maji kwenye Kata za Ruhunga, Mugajwale, Izimbya na Kikombero ambako kwa sasa wakazi wake wanahudumiwa na visima 23 vyenye uwezo wa kuhudumia watu 7,500 kati ya wakazi 11,794 waliopo katika Kata hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia awamu ya pili ya utekelezaji wa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji kwa Mwaka 2018/2019 imetenga shilingi bilioni 2.5 endapo Bunge litaridhia ili kuboresha zaidi upatikanaji wa huduma za maji Bukoba Vijijini ikiwemo maeneo yaliyotajwa na Mheshimiwa Mbunge.