Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 5 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 63 2018-02-05

Name

Dr. Raphael Masunga Chegeni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busega

Primary Question

MHE.DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:-
Migogoro ya ardhi na mipaka ya vijiji na hifadhi bado imeendelea kuwa tatizo sugu licha ya kuwepo kwa ahadi na kauli mbalimbali na Serikali.
Je, mgogoro wa Pori la Akiba Kijereshi na Sayanka katika Wilaya ya Busega utatatuliwa lini?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Raphael Masunga Chegeni, Mbunge wa Busega kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Pori la Akiba la Kijereshi lenye ukubwa wa kilometa za mraba 65.7 ililtangazwa rasmi na tangazo la Serikali Na. 215 la mwaka 1994. Pori hilo lilikabidhiwa rasmi kwa Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori mwaka 2005 kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Magu. Pori la Akiba la Kijereshi limepakana na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kwa upande wa Kaskazini na Kijiji cha Lukungu upande wa Mashariki, Mwamalole, Mwakiroba, Kijilishi, Igwata na Muungano upande wa Kusini Mashariki mwa pori hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, uvamizi wa mapori haya ya akiba kwa kilimo, makazi na ufugaji umesababisha ongezeko la matukio ya wanyamapori kuharibu mazao na kudhuru wananchi. Aidha, hali hii imesababisha migogoro baina ya wananchi na mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kutatua migogoro kati ya wakulima, wafugaji na maeneo ya hifadhi nchini Serikali imechukua hatua mbalimbali. Wizara kwa kushirikiana na wananchi imetambua na kuweka mipaka kwenye maeneo ya hifadhi ikiwemo Pori la Akiba la Kijereshi na Hifadhi ya Msitu wa Sayanka. Hadi mwisho wa Januari, 2018 jumla ya vigingi 74 vimesimikwa katika pori la Akiba Kijereshi, Aidha, katika Hifadhi ya Msitu wa Sayanka jumla ya vigingi 67 vimesimikwa, hatua hii imesaidia kupunguza migogoro ya mipaka kati ya wananchi na hifadhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, tatizo lililobaki kwa sasa ni baadhi ya wananchi kutaka kulima na kuanzisha makazi ndani ya Hifadhi ya Misitu ya Sayanka na wengine kutaka kulima ndani ya mita 500 kutoka mpaka wa Pori la Akiba la Kijereshi kinyume cha Sheria ya Misitu na Wanyamapori.
Wizara kwa kushirikiana na ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Busega na Halmashauri ya Wilaya ya Busega inaendelea kutoa elimu na kufanya vikao na mikutano na wananchi wanaozunguka Pori la Akiba Kijereshi. Mikutano hiyo inalenga kuwakumbusha wananchi umuhimu wa uhifadhi na kuepusha kufanya shughuli za kibinadamu ndani ya mita 500 kutoka mpaka wa pori la Akiba. Katazo hilo ni kwa mujibu wa Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori Namba 5 ya mwaka 2009. Aidha, Serikali inatoa wito kwa wananchi kuacha kuvamia maeneo ya hifadhi ili kudumisha uwepo wa bioanuai kwa faida yetu ya sasa na vizazi vijavyo. (Makofi)