Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 5 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 56 2018-02-05

Name

Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Primary Question

MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-
Katika Jimbo la Tunduru Kusini kuna vituo vitatu vya afya ambapo Kituo cha Afya Mtina kina zaidi ya miaka 30 hakijafanyiwa ukarabati na pia hakuna wodi ya wazazi.
Je, ni lini Serikali itajenga wodi ya wazazi katika kituo hicho na kufanya ukarabati ili kiweze kutoa huduma bora kwa wakazi wa Kata za Nasya, Semeni, Nyerere, Angalia na wakazi wa Kata ya Mchesi, Vijiji vya Likumbula, Tuwemacho na Namasakata?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ina vituo vitano ambapo vituo vya afya viwili vipo katika Jimbo la Tunduru Kusini na vitatu katika Jimbo la Tunduru Kaskazini. Kituo cha Afya Mtina kilianzishwa mnamo mwaka 1970 na kimekuwa kikiendelea kutoa huduma za kujifungua na huduma za matibabu ya kawaida kwa kipindi chote. Kwa sasa chumba cha kupumzikia akina mama baada ya kujifungua kimetengwa ndani ya wodi ya kawaida ya wanawake. Serikali kupitia wadau wa maendeleo (Walter Reed Program) waliweza kufanya ukarabati wa jengo la tiba na matunzo (CTC) kwa wagonjwa wanaoishi na virusi vya UKIMWI.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa msingi wa wodi ya wazazi katika Kituo cha Afya Mtina unaendelea kupitia fedha za Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo la Tunduru Kusini ambapo kiasi cha shilingi milioni nne zilitolewa. Aidha, Halmashauri katika bajeti ya mwaka wa fedha 2018/ 2019 imetenga kiasi cha shilingi milioni 10 kwa ajili ya ukarabati na kuboresha Kituo cha Afya Mtina.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, katika kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa Tunduru, Serikali kwa mwaka wa fedha 2017/2018 imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru kiasi cha shilingi milioni 400 kwa ajili ya ukarabati wa Kituo cha Afya Mkasale kilichopo katika Jimbo la Tunduru Kusini. Aidha, Halmashauri inajenga wodi mbili za upasuaji katika Hospitali ya Wilaya, nyumba ya mganga katika zahanati ya Naikula, ukarabati wa nyumba mbili za watumishi katika Kituo cha Afya Mchoteka na kuendeleza ujenzi wa zahanati ya Legezamwendo kupitia mapato yake ya ndani. Serikali itaendelea kuboresha vituo vya kutolea huduma za afya kwa kadri fedha zitakavyopatikana.