Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 4 Energy and Minerals Wizara ya Madini 44 2018-02-02

Name

Ester Alexander Mahawe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTER A. MAHAWE aliuliza:-
Madini ya Tanzanite yanachimbwa Mkoani Manyara katika Wilaya ya Simanjiro, lakini madini hayo huchakatwa na kuuzwa Mkoani Arusha hali inayosababisha wananchi wa Manyara kutofaidika kiuchumi.
(a) Je, ni nini kauli ya Serikali kuhusu kujenga kiwanda cha kuchakata madini hayo Mkoani Manyara?
(b) Je, ni kiasi gani cha fedha kimeshachangiwa na madini haya katika mapato ya Mkoa wa Manyara?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Madini, naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Ester Alexander Mahawe, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Manyara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha kuwa madini ya Tanzanite yananufaisha wananchi wa Simanjiro, Serikali imetoa tamko la kutaka shughuli zote zinazohusu madini ya Tanzanite ikiwemo uendeshaji wa minada na ujenzi wa viwanda vya uchakataji wa madini hayo zifanyike katika eneo la Mererani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali imetenga eneo katika Kijiji cha Naisinyai, Mererani ili kuwa eneo maalum kiuchumi kwa ajili uanzishaji wa viwanda vya uchakataji (Economic Processing Zone - EPZ) ili kuvutia uwekezaji katika eneo hilo kwa kutoa vivutio mbalimbali kwa wawekezaji. Hivyo Wizara itaendelea kuhamasisha wawekezaji wa viwanda vya kuchakata madini ya Tanzanite kujenga viwanda katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza hilo kwa vitendo, Wizara ya Madini imepata kiwanja katika eneo la EPZ ili kujenga Kituo cha Umahiri (Center of Excellence), sehemu ya jengo hilo itakuwa na taasisi mbalimbali zinazosimamia shughuli za madini ili kutoa huduma kwa wafanyabiashara wa madini ya Tanzanite kwa haraka (One Stop Centre). Pia baadhi ya ofisi katika jengo hilo litatumika kutoa huduma za uthaminishaji wa madini na kuendesha minada.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwaka 2015 hadi 2017 madini ya Tanzanite yamechangia kiasi cha shilingi 140,954,229.37 kutokana na kodi ya tozo ya huduma (Service Levy) inayotozwa mujibu wa Sheria ya Ushuru wa Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, manufaa mengine yaliyopatikana kwa Wilaya ni pamoja na fursa za ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja kutokana na kuwepo kwa migodi katika eneo husika na huduma za jamii zinazotolewa na mgodi ambapo mgodi umetoa ajira kwa wafanyakazi 674 ambapo asilimia 93 ya walioajiriwa ni Watanzania na asilimia saba iliyobaki ni wageni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya waajiriwa hao, asilimia 21.81 ya wafanyakazi wameajiriwa katika vijiji kutoka vijiji vinavyozunguka mgodi vya Naisinyai na Mererani. Katika kipindi hicho mgodi wa Tanzanite One umefanikiwa kuchangia jumla ya dola za Kimarekani 429,664 katika utoaji wa huduma mbalimbali za kijamii ukilenga kuimarisha mahusiano na jamii zinazozunguka mgodi pamoja na kuchangia maendeleo ya Taifa kwa ujumla. Huduma hizi zinahusisha masuala ya elimu, afya, lishe, ujenzi na sanaa.