Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 3 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 34 2018-02-01

Name

Ussi Salum Pondeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chumbuni

Primary Question

MHE. USSI SALUM PONDEZA aliuliza:-
Katiba ya Jamhuri ya Muungano inatambua uwepo wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.
(a) Je, kwa nini ripoti za Tume hiyo hazitolewi kwa muda muafaka kila mwaka kama masharti ya Katiba yanavyosema?
(b) Je, ripoti ya mwisho ya Tume hiyo ilitolewa mwaka gani na lini imewasilishwa Bungeni?
(c) Je, kwa nini harakati za Tume hiyo katika kushughulikia migogoro ya ardhi, ukaguzi wa vituo vya polisi, magereza pamoja na matukio ya uvunjaji wa haki za binadamu umezorota kinyume na miaka ya nyuma?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ussi Salum Pondeza, Mbunge wa Chumbuni, kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 131(3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaelekeza Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kuwasilisha taarifa zake kwa Waziri mwenye dhamana ya masuala ya haki za binadamu ambaye hutakiwa kuwasilisha taarifa hizo nbele ya Bunge mapema iwezekanavyo. Taarifa hizo ni muhtasari wa masuala yote yaliyofanyika katika mwaka husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa huko nyuma taarifa za Tume zilikuwa zikichelewa kuwasilishwa Bungeni kwa wakati. Hata hivyo, mwezi Desemba, 2017, Tume imewasilisha taarifa zake za nyuma hadi mwaka 2014/2015 kwa Waziri mwenye dhamana ili aziwasilishe Bungeni. Taarifa ya mwaka 2015/2016 ipo katika hatua ya mwisho ya uchapaji na itakapokuwa tayari itawasilishwa kwa Waziri mwenye dhamana. Taarifa ya mwaka 2016/2017 ipo katika maandalizi na inasubiri kukamilika kwa taarifa ya ukaguzi wa hesabu za Tume.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya mwisho iliyotolewa na kuwasilishwa Bungeni ilikuwa ya kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo, kweli kwamba utendaji wa Tume umezorota, Tume imeendelea kufanya kazi zake kama zilivyoainishwa katika Katiba na Sheria. Aidha, Tume imekuwa ikiongeza jitihada kila mwaka kukagua vituo vya polisi, magereza, vituo vya mafunzo kwa upande wa Zanzabar, kufuatilia migogoro ya ardhi na kufuatilia utekelezaji wa haki za binadamu na misingi ya utawala bora kwa ujumla. Lengo kuu la ukaguzi na ufuatiliaji huu ni kutathmini hali ya haki za binadamu na misingi ya utawala bora na kutoa mapendekezo kwa taasisi husika. Vilevile Tume imekuwa ikifuatilia utekelezaji wa haki za makundi mbalimbali ambayo ni pamoja na watoto hususani watoto walio katika mkinzano na sheria, wanawake na watu wenye ulemavu.