Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 2 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 25 2018-01-31

Name

Emmanuel Adamson Mwakasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Primary Question

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA,aliuliza:-
Kumekuwa na migogoro mingi ya ardhi nchini inayosababisha uvunjifu wa amani miongoni mwa wananchi na hata katika baadhi ya maeneo migogoro hiyo imesababisha vifo;
(a) Je, Serikali imechukua hatua gani kutatua migogoro hiyo?
(b) Kwa kuwa Maafisa Ardhi wengi ndiyo chanzo cha migogoro hiyo, je, ni Maafisa Ardhi wangapi wamechukuliwa hatua kwa kusababisha migogoro hiyo?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uniruhusu kwanza kwa sababu ni mara ya kwanza mwaka huu niwatake heri ya mwaka mpya wote na tumshukuru Mungu kwamba tunaendelea kulijenga Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Emanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uwepo wa migogoro ya ardhi nchini na tayari imeweka mikakati mbalimbali ya kuitatua na kuzuia uwezekano wa kuibuka migogoro mipya. Baadhi ya mikakati hiyo ni pamoja na:-
(i) Kutoa elimu kwa watendaji wanaohusika na utatuzi wa migogoro ya ardhi kuanzia ngazi za Serikali za Mitaa hadi Serikali Kuu na kuzifanyia marekebisho sera na sheria mbalimbali zinazosimamia sekta ya ardhi;
(ii) Kuboresha Mabaraza ya Ardhi na kuyaongezea watumishi pamoja na vitendea kazi;
(iii) Kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi ya wilaya na vijiji; na
(iv) Kutekeleza mkakati wa kupima kila kipande cha ardhi nchini na kuboresha mifumo ya kutunza kumbukumbu za ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Wizara imeanzisha utaratibu wa kushughulikia migogoro ya ardhi ambapo Mheshimiwa Waziri akiambatana na wataalam wa sekta ya ardhi amekuwa akikutana na wananchi papo kwa papo na kutatua migogoro na changamoto zinazowakabili kwa mfumo ambao tunaita Funguka na Waziri wa Ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya ardhi kwa namna moja ama nyingine husababisha pia na watendaji wa sekta ya ardhi wasio waaminifu; lakini Serikali imeendelea kuwachukulia hatua maofisa hao kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya mwaka 2014/2015 na 2016/2017, watumishi wanne wamesimamishwa kazi baada ya kufikishwa Mahakamani kutokana na ukiukwaji wa maadili ya Utumishi wa Umma; watumishi 16 walifukuzwa kazi kwa makosa mbalimbali ya kiutendaji; na watumishi 19 waliandikiwa barua za onyo na kutakiwa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zinazoongoza utumishi wa umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa watendaji wa sekta ya ardhi walio chini ya usimamizi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa Wizara imekuwa ikishirikiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI katika kuhakikisha kuwa hatua stahiki zinachukuliwa dhidi ya watendaji hao ambao wamekuwa wakisababisha migogoro kutokana na kutowajibika au kukiuka masharti ya ajira zao.