Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 20 2018-01-31

Name

Magdalena Hamis Sakaya

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Kaliua

Primary Question

MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka mradi wa TASAF awamu ya III katika vijiji ambavyo havijapata mradi katika Jimbo la Kaliua?

Name

Capt. (Mst). George Huruma Mkuchika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Newala Mjini

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, UTUMISHI NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa dada yangu Magdalena Hamis Sakaya, Mbunge wa Kaliua, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa kunusuru kaya maskini ambao umo ndani ya TASAF awamu ya III unaendelea na utekelezaji wake katika halmashauri 159 pamoja na Unguja na Pemba. Mpango wa kunusuru kaya masikini una sehemu tatu ambazo ni uhaulishaji fedha kwa kutimiza masharti ya elimu na afya kwa watoto walioko shuleni na wale wanaotakiwa kuhudhuria kliniki pamoja na walengwa kufanya kazi za ajira ya muda. Sehemu nyingine ni kukuza uchumi wa kaya kwa kuweka akiba na kuanzisha miradi ya kuongeza kipato na uboreshaji wa miundombinu ya elimu na afya ili kuwawezesha walengwa kutimiza masharti ya elimu na afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa kunusuru kaya maskini unatekelezwa katika halmashauri 159 za Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar kwa maana ya Unguja na Pemba lakini si katika vijiji, mitaa na shehia zote. Mpango ulipoanza utekelezaji mwaka 2013, rasilimali zilizokuwepo zilitosheleza kufikia asilimi 70 tu ya maeneo yote, ambayo ni sawa na vijiji, mitaa, shehia 9,989 na maeneo yaliyobaki yana vijiji, mitaa, shehia zaidi ya 5000. Kila halmashauri nchini imegusa kwa wastani wa asilimia 30 ya maeneo yake ambayo hayajafikiwa na mpango wa kunusuru kaya maskini na hili si kwa Jimbo la Kaliua pekee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba yapo maeneo yenye kaya zenye vigezo vya umaskini na uhitaji ambavyo bado havijafikiwa. Serikali ipo katika hatua za mwanzo za kuanza kuandaa sehemu ya pili ya TASAF awamu ya tatu ambayo itaendelea kwa miaka mingine mitano. Lengo la sehemu hii ya pili ni kuzifikia kaya zote maskini nchini na kuimarisha utekelezaji wa mpango na kuwasaidia wananchi kuwa na shughuli za kiuchumi na uzalishaji zaidi ili waweze kuondokana na umaskini.