Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 1 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 13 2018-01-30

Name

Venance Methusalah Mwamoto

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Primary Question

MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-
Je, ni kiasi gani cha fedha kinatolewa kwa Wilaya ambazo zinapakana au zilizo na Hifadhi za Taifa ikiwamo Wilaya ya Kilolo katika Hifadhi ya Udzungwa?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Mwamoto, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maliasili na Utalii, kupitia Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA), inatekeleza Mpango wa Ujiarni Mwema (Support for Community Initiated Projects) ulioanzishwa mapema miaka ya 1990. Lengo la mpango huu ni kuishirikisha jamii katika kupunguza changamoto za uhifadhi na kuwanufaisha wananchi waishio jirani na hifadhi. Utekelezaji wa Mpango wa Ujirani Mwema unahusisha vijiji katika Wilaya zinazopakana na Hifadhi za Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa, vijiji vinaibua miradi ya maendeleo na kuchangia asilimia 30 ya gharama za miradi na shirika kuchangia asilimia 70 ya gharama hizo. Kupitia mpango huu kila mwaka TANAPA inatenga kati ya 5% hadi 7% ya bajeti yake kwa shughuli za miradi hiyo. Vilevile mpango huu unahusisha utoaji wa elimu ya uhifadhi na kuwashirikisha wananchi katika uhifadhi wa maliasili na mazingira kama vile upandaji wa miti na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha kuanzia mwaka 2000/2001 hadi mwaka 2017/2018 Hifadhi ya Taifa ya Udzungwa imefanikiwa kutekeleza miradi ya ujirani mwema katika Wilaya ya Kilolo yenye thamani ya jumla ya shilingi 435,962,656. Baadhi ya miradi iliyotekelezwa na inayoendelea kutekelezwa Wilaya ya Kilolo inahusu uwekaji wa umeme, ujenzi wa barabara, ununuzi wa samani na ununuzi wa vifaa vya maabara vya Sekondari ya Lukosi katika Kijiji cha Mtandika ambapo jumla ya shilingi 49,460,937 zimetumika.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa nyumba wa awamu za walimu katika Kijiji cha Ikura umegharimu shilingi 60,000,000; ukarabati barabara ya Ilula – Udekwa, ujenzi na ununuzi wa samani Kituo cha Polisi, nyumba ya walimu, shule ya msingi katika Kijiji cha Udekwa umegharimu shilingi 227,501,719 na mpango wa matumizi bora ya ardhi na nyumba ya walimu shule ya msingi Msosa katika Kijiji cha Msosa shilingi 81,000,000 na ununuzi wa madawati kwa ajili ya Wilaya ya Kilolo umegharimu shilingi 18,000,000. Jumla ya fedha zote zilizotolewa na Shirika ni shilingi 435,962,656.