Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 9 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 107 2017-11-17

Name

Dr. Dalaly Peter Kafumu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igunga

Primary Question

DKT. DALALY P. KAFUMU aliuliza:-
Zaidi ya asilimia 70 ya eneo la Jimbo la Igunga lilikuwa limefunikwa na maji ya Ziwa Victoria lakini baada ya Ziwa hilo kukauka, eneo hilo limebaki kuwa ni mbuga inayojaa maji wakati wa masika hivyo kufanya ujenzi wa barabara za vijiji kuwa wa gharama kubwa sana na Halmashauri ya Wilaya ya Igunga haina uwezo wa kifedha kujenga barabara hizo.
Je, kwa nini Serikali isiandae mradi mkubwa wa ujenzi wa barabara za vijijini katika Wilaya ya Igunga na Wilaya nyingine nchini zenye tatizo kama hili?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu, Mbunge wa Jimbo la Igunga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kutatua tatizo la udongo, Serikali kupitia Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini yaani TARURA imepanga kufanya utafiti wa udongo huo ili kuona kama unafaa baada ya kuongezewa kemikali (additive) badala ya kuondoa na kuleta udongo mwingine na hivyo kupunguza gharama za ujenzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Halmashauri ili ziweze kupitika kwa kipindi chote. Katika mwaka wa fedha 2016/17 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Igunga shilingi milioni 336.8 ambazo zilitumika kufanya matengenezo ya barabara kilometa 119.3, madaraja 8 na kalvati 10. Vilevile katika mwaka wa fedha 2017/18 Hamashauri hiyo imetengewa shilingi bilioni 1.26 ambapo hadi tarehe 30 Septemba, 2017 fedha zilizopokelewa ni shilingi milioni 241.9. Taratibu na kumpata mkandarasi zinaendelea.