Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 8 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 99 2017-11-16

Name

Elibariki Emmanuel Kingu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Magharibi

Primary Question

MHE. ELIBARIKI I. KINGU aliuliza:-
Uandaaji wa Mashindano ya Kimataifa ya Mpira wa Miguu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu la Afrika (CAF) unataka Miji miwili iteuliwe kuendesha mashindano hayo:-
Je, Serikali imeteua mji upi wa pili mbali na Dar es Salaam kuendeshea Mashindano ya AFCON ya vijana chini ya umri wa miaka 17 ya mwaka 2019 yatakayofanyika Tanzania?

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa sababu leo ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge lako Tukufu, naomba kwanza nichukue nafasi hii kuweza kumshukuru Mwenyezi Mungu. Kwa kipekee kabisa nichukue nafasi hii kuweza kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Pombe Magufuli kwa imani yake kubwa ambayo ameionesha kwangu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa kipekee kabisa nikushukuru wewe mwenyewe Naibu Spika pamoja na Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mchango wenu na ushirikiano wote ambao mlikuwa mkinipa kipindi nikiwa Mbunge. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako pia naomba nichukue nafasi hii kuweza kuwapa pole wazazi, wanafunzi pamoja na Walimu wa Nduda iliyopo katika Mkoa wangu wa Songwe kwa kuondokewa na wanafunzi ambao walifariki baada ya kupigwa na radi wakiwa shuleni. Nawaombea Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi. Amina.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Elibariki Kingu, Mbunge wa Singida Magharibi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, uteuzi wa maeneo ya nchi yetu yatakayotumika kuendesha mashindano ya AFCON mwaka 2019 kwa vijana chini ya umri wa miaka 17, utafanywa na Kamati ya Maandalizi ya Mashindano ya AFCON 2019 iliyotangazwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo siku ya Jumamosi tarehe 11/11/2017 Jijini Dar es Salaam.
Mheshimiwa Spika, maandalizi ya mashindano haya ukiwemo uteuzi wa maeneo ya kuendeshea mashindano hayo, ni sehemu ya hadidu za rejea za Kamati hiyo ambayo Mwenyekiti wake ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. Makamu wake ni Mjumbe wa Kamati Tendaji ya Shirikisho la Soka la Afrika (CAF) ndugu Leodger Tenga na Mtendaji wake mkuu ni Makamu wa Rais wa Kamati ya Olimpiki ya Tanzania, ndugu Henry Tandau.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kazi kubwa inayoikabili Kamati hii ni uboreshaji wa miundombinu kwa viwango vya Kimataifa, kazi ya uteuzi wa maeneo ya kuendeshea mashindano hayo itafanyika mapema iwezekanavyo. (Makofi)