Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 5 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 56 2017-11-13

Name

Esther Nicholus Matiko

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:-
Kufuatia utoaji wa elimu ya msingi bure, shule za msingi na sekondari ndani ya Halmashauri ya Mji wa Tarime zimekuwa na upungufu mkubwa wa madarasa na madawati hadi kufikia walimu kulazimika kufundishia chini ya mti na wanafunzi walio madarasani wanakaa kwenye sakafu kwa idadi kubwa kinyume na matakwa ya Sera ya Elimu.
Je, ni nini mpango wa Serikali wa kuhakikisha shule hizo ndani ya Halmashauri ya Mji wa Tarime zinaondokana na changamoto za miundombinu ya kufundishia na kujifunzia ili kutoa elimu bora?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya miundombinu ya elimu nchini ni matokeo ya mwitikio mkubwa wa wananchi katika utekelezaji wa Mpango wa Elimu Bila Malipo ambao umetoa fursa kwa watoto wote wenye umri wa kwenda shule kupata fursa hiyo. Shule 30 za msingi katika Halmashauri ya Mji wa Tarime zinahitaji vyumba vya madarasa 625, vyumba vya madarasa vilivyopo ni 215 na upungufu ni vyumba vya madarasa 410. Aidha, madawati yanayohitajika ni 8,888; madawati yaliyopo ni 6,066 na upungufu ni madawati 2,823.
Mheshimiwa Mwenyekiti, shule nane za sekondari katika Halmashauri ya Mji wa Tarime zinahitaji kuwa na vyumba vya madarasa 133, madarasa yaliyopo ni 104 ma upungufu ni madarasa 29. Aidha, katika shule hizo kuna ziada ya madawati 421 kutokana na mwitikio mzuri wa wananchi na jitihada za Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo kupitia fedha za kuchochea Maendeleo ya Mfuko wa Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imetenga shilingi 119,000,000.00 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa vyumba vya madarasa 16, matundu 19 ya vyoo na kuongeza madawati 154 katika shule za msingi. Vilevile Serikali imetenga shilingi 172,500,000 kupitia ruzuku ya maendeleo na mapato ya ndani kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa 22 na matundu ya vyoo 72.