Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 5 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 55 2017-11-13

Name

Ezekiel Magolyo Maige

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Msalala

Primary Question

MHE. EZEKIEL M. MAIGE aliuliza:-
Wananchi wa Jimbo la Msalala kwa kusaidiana na Mbunge wao wameanza ujenzi wa Vituo vya Afya Bugarama, Mega, Ngaya na Isaka na miradi hiyo ipo katika hatua nzuri.
(a) Je, Serikali imejipangaje kusaidia miradi hiyo ya ujenzi wa Vituo vya Afya?
(b) Je, Serikali imejipangaje kukamilisha maboma zaidi ya 28 ya zahanati kwenye vijiji mbalimbli Jimboni Msalala?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama hapa kujibu maswali, naomba uniruhusu nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kunijalia afya na nguvu kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Pili, naomba nimshukuru Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Uongozi wote wa Bunge kwa malezi na maelekezo ambayo nimepata, bila kusahau Kamati ya Bajeti, chini ya Uenyekiti wa Mheshimiwa Hawa Ghasia kwa malezi na ushirikiano ambao nimekuwa nikiupata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee naomba nimshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa imani yake kwangu kwa kuniteua kuhudumu katika nafasi ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais – TAMISEMI. Uteuzi uliopokelewa kwa mikono miwili kwa wananchi wa Kalambo na Mkoa wa Rukwa kwa ujumla wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kutoa pongezi zangu za dhati kwa Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Msalala kwa jitihada anazofanya katika kuwahamasisha wananchi wake kuibua na kuanzisha miradi mingi ya ujenzi wa vituo vya kutolea huduma za afya katika Jimbo lake la Msalala.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala ina jumla ya vituo vya afya vitatu ambavyo ni Lunguya, Chela pamoja na Bugarama vilivyosajiliwa kwa mujibu wa sheria. Kati ya vituo hivyo, ni vituo viwili ambavyo ni Kituo cha Afya cha Lunguya na Chela ndivyo vinavyotoa huduma za upasuaji wa dharura kwa akina mama wajawazito.
Aidha, ujenzi wa vituo vingine vitatu ambavyo ni Isaka, Ngaya na Mega upo kwenye hatua mbalimbali za ujenzi ambapo lengo la Serikali ni kuwa ifikapo mwaka 2020 vituo hivi viwe vimekamilisha miundombinu muhimu inayohitajika kustahili kuwa vituo vya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala ina jumla ya maboma 31. Miongoni mwa maboma hayo, matatu ni vituo vya afya tarajiwa ambavyo ni Isaka, Mega na Ngaya. Aidha, kwa sasa Vituo vya Mega na Ngaya maboma yamepauliwa katika jengo la wagonjwa wa nje (OPD) ambapo Boma la Kituo cha Afya cha Isaka lipo kwenye hatua za lenta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali iliweza kukamilisha ujenzi wa zahanati mpya nne kwa gharama ya kiasi cha shilingi milioni 277 na saba ambazo zote zipo katika kata ambazo zilikuwa hazina huduma za afya kabisa. Zahanati hizo zipo katika Vijiji vya Nyaminje, Mbizi, Mwanase na Mwakata ambapo kukamilika kwake kumepunguza adha ya wananchi kutembea umbali mrefu kutafuta huduma ya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika mpango wa kitaifa wa kuboresha vituo vya afya kwa ajili ya kutoa huduma za dharura kwa upasuaji wa akina mama, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala imepatiwa kiasi cha shilingi milioni 400 kutoka Serikali Kuu kwa ajili ya kujenga wodi ya wanawake, nyumba ya watumishi, jiko, jengo la kuhifadhia maiti na ukarabati wa miundombinu ya nyumba za watumishi iliyochakaa katika Kituo cha Afya cha Chela. Kituo cha Afya cha Chela tayari kina jengo la upasuaji, wodi ya wazazi, maabara, kichomea taka, shimo la kutupia kondo la nyuma na mfumo wa maji safi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo katika bajeti ya mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imetenga kiasi cha shilingi 336,742,394 za ruzuku ya maendeleo( CDG) kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati katika vijiji saba vya Nyamigege, Gula, Ikinda, Kalole, Jomu, Buchambaga na Ndala, kati ya hayo maboma 31.