Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 6 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 53 2016-04-27

Name

Haroon Mulla Pirmohamed

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbarali

Primary Question

MHE. HAROON M. PIRMOHAMED aliuliza:-
Katika GN. Na. 28 ya mwaka 2008 inawataka wananchi wanaoishi katika vijiji 21 vilivyopo katika Jimbo la Mbarali, Wilaya ya Mbarali, Mkoani Mbeya wahame ili kupisha Hifadhi ya Taifa ya Ruaha ingawa wananchi katika vijiji hivyo wameishi katika maeneo hayo tangu enzi za mababu zao:-
Je, ni lini Serikali itafuta GN. Na. 28 ya mwaka 2008 ili wananchi katika vijiji hivyo waweze kuishi bila kubughudhiwa pamoja na kuendelea na shughuli zao za kilimo na ufugaji?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Haroon Mulla Pirmohamed, Mbunge wa Mbarali, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, tangazo la Serikali Na. 28 la mwaka 2008 lilihusu kuhifadhiwa Bonde la Usangu kama sehemu ya Hifadhi ya Taifa ya Ruaha hatua ambayo ulihusisha kutunza vyanzo vya maji kwa ajili ya shughuli za kilimo na kibinadamu, uzalishaji wa umeme na matumizi ya kiikolojia kwa maslahi mapana ya kitaifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wanaoishi katika vijiji 21 vilivyopo katika Jimbo la Mbarali, Wilaya ya Mbarali, Mkoani Mbeya wamewasilisha malalamiko yao Serikalini wakipinga uhalali wa mpaka mpya uliotokana na Tangazo la Serikali nililolitaja na hivyo kuendelea kuwepo ndani ya mpaka. Aidha, baadhi ya wananchi waliotii sheria na kuondoka katika maeneo husika wamelalamikia viwango vya fidia vilivyolipwa katika kipindi cha mwaka 2006 hadi 2008 baada ya taratibu zote za kiserikali ikiwemo kufanya tathmini kukamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikifanya kila jitihada kutatua mgogoro huo katika ngazi mbalimbali ikiwemo vikao vya ushauri baina ya wadau wakiwemo wananchi katika eneo husika, uongozi wa Wilaya ya Mbarali na Mkoa wa Mbeya, Wizara ya Maliasili na Utalii na Ofisi ya Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iliunda timu ya wataalam na kupitia upya mipaka iliyotangazwa ili kutoa ushauri wa kitaalam juu ya mipaka hiyo na kuwasilisha ripoti kwenye Kamati ya pamoja kati ya Mkoa wa Mbeya na Wizara ya Maliasili na Utalii na kuhakiki malipo ya fidia kwa wananchi waliohama kupisha eneo lililojumuishwa kwenye Hifadhi ya Taifa Ruaha.
Mheshimiwa Naibu Spika, uhakiki huo ulikusudia kuondoa malalamiko ya mapunjo yaliyojitokeza kutoka kwa baadhi ya wananchi, kupitia na kuhakiki maeneo yote ya mpaka ardhini ili kujua maeneo gani yataathiriwa na mpaka mpya na kuona ni kwa namna gani mpaka utaweza kurekebishwa bila kuathiri lengo kuu la kuhifadhi sehemu ya eneo hilo la Bonde la Usangu. Mapedekezo yatakayotokana na kazi hii yatatumika kufanya maamuzi sahihi juu ya mipaka ya eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kusisitiza kuwa eneo la Bonde la Usangu, lililotajwa kwenye GN. Na. 28 ya mwaka 2008 ni eneo linalolindwa kisheria na umuhimu wake bado uko pale pale. Hivyo, badiliko lolote la mipaka ndani yake litahitajika kufanyika kwa kuzingatia taratibu za kisheria kupitia Bunge lako Tukufu.