Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 4 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 45 2017-11-10

Name

Angelina Adam Malembeka

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza:-
Kutokana na uvamizi wa ardhi katika maeneo ya mashule, masoko na zahanati.
(a) Je, ni lini Serikali itakamilisha upimaji wa maeneo hayo?
(b) Je, kutokana na ukubwa wa gharama za upimaji, kwa nini zoezi la upimaji lisitolewe bure kwa taasisi za umma kupitia Halmashauri hizo?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya shule, soko, zahanati, vituo vya afya, hospitali, vyuo, ofisi za Serikali, vituo vya polisi, mahakama, maeneo ya majeshi, hifadhi za misitu na wanyama na maeneo ya makumbusho hutengwa maalum kwa ajili ya matumizi ya umma na shughuli mbalimbali za Serikali. Maeneo yote haya yapo chini ya usimamizi na uangalizi wa Mamlaka ya Serikali za Mitaa au Serikali Kuu. Hata hivyo, maeneo mengi kati ya hayo yamekuwa yakisimamiwa na taasisi za Serikali bila kupimwa wala kuwa na hatimiliki badala yake yamekuwa yakimilikishwa kwa utaratibu wa kupewa government allocation.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu huu pamoja na kwamba umekuwa ukifanywa kwa nia njema, umetoa mwanya kwa wananchi wenye nia ovu kuyavamia, kuyamega na kuyaendeleza maeneo ya Serikali kinyume na utaratibu. Ili kuhakikisha kuwa changamoto ya uvamizi wa maeneo ya umma unakomeshwa, Serikali kupitia Wizara yangu iliagiza kuwa maeneo yote ya umma, yapimwe na yamilikishwe kwa taasisi husika kupitia barua yenye Kumb. Na. AB225/30/305/01 ya tarehe 7 Septemba, 2016.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuitikia wito huu baadhi ya taasisi za Serikali ikiwemo TBA, Hazina na TANROADS zinaendelea kuyatambua maeneo yake na kuyamilikisha maeneo wanayoyasimamia. Nitoe rai kwa Wakuu wote wa taasisi za umma kuhakikisha wanakamilisha zoezi hili mapema na kwa maeneo ambayo yamevamiwa ni vema wavamizi wakaondoka kwa hiari yao na wasisubiri mkondo wa sheria uwakumbe. Aidha, nampongeza sana Mkuu wa Mkoa wa Tabora na timu yake kwa kutekeleza agizo la Waziri kwa vitendo na ni vema Wakuu wote wa Mikoa wengine wakachukua hatua ili kuondoa wavamizi kwenye maeneo yote ya umma.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama elekezi za huduma za upimaji ambazo kwa mara ya mwisho zilifanyiwa mapitio mwaka 2016 siyo kubwa kama inavyodhaniwa kwa kuwa upimaji wa ardhi hufanywa kwa misingi ya kurejesha gharama pakee. Gharama hizo hujumuisha vifaa vya upimaji, shajara, usafiri, matengenezo ya vifaa na mawasiliano ya kitaalam. Aidha, kukamilika kwa mtandao wa upimaji (Taref 11) tutasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza gharama za upimaji nchini.
Mheshimia Mwenyekiti, natoa rai kwa taasisi zote za Serikali nchini kuhakikisha zinapima na kumilikishwa maeneo yao ili kuwa na miliki salama kwa kuwa ulinzi wa ardhi wanayomilikishwa ni jukumu la taasisi husika. Aidha, taasisi zote za umma nchini zinahimizwa kutenga fedha katika bajeti zao kwa ajili ya kuharakisha upimaji wa maeneo yote wanayoyasimamia.