Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 4 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 44 2017-11-10

Name

Lucia Ursula Michael Mlowe

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-
Msongamano wa magari, ujenzi holela, miundombinu duni ya maji taka na kadhalika katika miji mikubwa hapa nchini vinatokana na udhaifu wa upangaji wa matumizi bora ya ardhi (poor land use planning).
Je, Serikali imejiandaa vipi kuendesha zoezi la Mipango Miji na matumizi bora ya ardhi katika miji mipya ikiwemo Halmashauri ya Mji wa Njombe?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu Namba 7(1) cha Sheria ya Mipango Miji Na. 8 ya mwaka 2007 kinaelekeza kuwa jukumu la upangaji na uendelezaji miji lipo chini ya mamlaka za upangaji ambazo ni Halmashauri za Majiji, Manispaa Miji, Wilaya na Mamlaka za Miji Midogo. Kutokana na umuhimu wa kuwa na Miji iliyopangwa kiuchumi na kijamii, Serikali imechukua hatua mbalimbali ikiwemo uandaaji wa mipango kabambe itakayotumika kuongoza, kusimamia na kudhibiti uendelezaji wa Miji pamoja na urasimishaji wa makazi yasiyopangwa katika maeneo mbalimbali nchini.
Hadi kufikia Oktoba 20, 2017 maandalizi ya mipango kapambe ya miji 29 nchini ilikuwa imefikia katika hatua mbalimbali. Maeneo hayo ambayo tayari mipango yake ipo katika hatua mbalimbali ni Majiji ya Mwanza, Da es Salaam, Arusha na Tanga na kwa upande wa Manispaa tunayo Mtwara - Mikindani, Iringa, Musoma, Tabora, Singida, Sumbawanga, Songea, Shinyanga, Morogoro, Lindi, Bukoba, Moshi, Mpanda na Kigoma Ujiji. Kwa upande wa miji midogo ni Kibaha, Korogwe, Njombe, Bariadi, Geita, Babati, Ifakara, Mahenge, Malinyi, Tunduma na Mafinga. Kati ya maeneo hayo, mipango kabambe kwa Manispaa ya Mtwara - Mikindani, Musoma, Iringa na Singida imeshaidhinishwa na kuzinduliwa na hivyo imeanza kutumika rasmi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uandaaji wa mipango kabambe hufanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali yakiwemo makampuni ya upangaji na upimaji ardhi yaliyosajiliwa kwa mujibu wa sheria, wamiliki wa ardhi, taasisi za Serikali, watu binafsi na asasi za kiraia pamoja na taasisi, zinatoa huduma mbalimbali za miundombinu kama vile TANESCO, TANROADS na Mamlaka za Maji Safi na Maji Taka. Utekelezaji wa mipango hiyo husaidia kutatua changamoto zilizopo na hatimae kuwa na miji iliyopangwa na yenye mtandao mzuri wa miundombinu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango kabambe wa Mji wa Njombe unaandaliwa na Kampuni ya CRM Land Consult ya Dar es Salaam kupitia programu ya Urban Local Government Strengthening Program iliyofadhiliwa na Benki ya Dunia chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Hadi sasa rasimu ya kwanza ya mpango kabambe ya mji huo imeandaliwa na hatua inayofuata ni kuwasilisha rasimu hiyo kwenye mikutano ya wadau kwa ajili ya kupokea maoni na mapendekezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa wito kwa mamlaka za upangaji ambazo hazina mipango kabambe, kuanza maandalizi ya mipango hiyo pamoja na kongeza kasi ya kupanga maeneo mapya, kurasimisha makazi yasiyopangwa na kudhibiti uendelezaji holela kwa kushirikiana na makampuni yaliyosajiliwa kufanya kazi hiyo kwa mujibu wa sheria.