Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 2 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 20 2017-11-08

Name

Mary Deo Muro

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARY D. MURO aliuliza:-
Tangu mwaka 2014 TANESCO iliweka alama ya X kwenye maeneo ya Kiluvya, Kibaha hadi Chalinze kupisha ujenzi wa kupitisha umeme wa Gridi ya Taifa lakini hadi sasa hakuna fidia iliyolipwa kwa wananchi hao na pia wanashindwa kufanya uendelezaji wa maeneo hayo. Je, ni lini wananchi hao watalipwa fidia stahiki?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mary Deo Muro, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO inatekeleza mradi mkubwa wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 400 kutoka Kinyerezi Dar es Salaam kupitia Chalinze, Segera hadi Arusha yenye urefu wa kilometa 600. Pia mradi huo utahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wenye msongo wa kilovoti 220 kutoka Kibaha hadi Bagamoyo yenye urefu wa kilometa 40 na kutoka Segera hadi Tanga yenye urefu wa kilometa 60. Mradi huu pia unahusisha ujenzi wa vituo vya kupoozea umeme vya Chalinze, Segera, Kange na Zinga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, malengo ya mradi huu ni kuongeza upatikanaji wa umeme katika Ukanda wa Mashariki na Kaskazini mwa nchi kutoka kwenye mitambo ya kuzalisha umeme ya Kinyerezi. Gharama za mradi huo ni dola za Marekani milioni 693 ambazo zitagharamiwa kwa mkopo kutoka benki ya Exim-China kwa asilimia 85 na Serikali ya Tanzania asilimia 15.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kutathmini mali za wananchi watakaopisha mradi huo kutoka Kibaha hadi Chalinze imekamilika na kuidhinishwa na Mtathmini Mkuu wa Serikali. Jumla ya shilingi bilioni 21.6 zitahitajika kwa ajili ya kulipa fidia kwa wananchi wapatao 855 wa Halmashauri za Kisarawe, Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini, Bagamoyo ikiwemo eneo la Kiluvya. Fidia hiyo italipwa na Serikali na fedha hizo zimetengwa katika bajeti ya Wizara kwa mwaka 2017/2018. Taratibu zote za uandaaji taarifa na majedwali ya malipo ya fidia zimekamilika na malipo yamepangwa kulipwa katika mwaka huu wa fedha 2017/2018.