Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 34 Defence and National Service Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa 276 2017-05-25

Name

Lucy Simon Magereli

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CECILIA D. PARESSO (K.n.y. MHE. LUCY S. MAGERELI) aliuliza:-
Askari wa JWTZ wamekuwa wakijichukulia sheria mkononi kwa kutesa raia na saa nyingine Jeshi la Polisi. Matukio haya yamekuwa yakifanyika maeneo ya starehe, kwenye foleni za magari, mitaani na katika magari ya usafiri wa umma. Hivi karibuni Mkoani Tanga, kijana mmoja kondakta wa daladala alimzuia mtoto wa mwanajeshi kupanda daladala yake bila nauli, alikamatwa na kuteswa na wanajeshi ndani ya Kambi, kitu kilichopelekea kifo chake.
(a) Je, sheria ipi inawapa wanajeshi haki ya kutesa raia?
(b) Je, Serikali inachukua hatua gani kukomesha hali hii?

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucy Simon Magereli, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hakuna sheria yoyote inayowapa haki wanajeshi kutesa raia au kuvunja sheria.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, matukio ya wanajeshi kushambulia raia au raia kushambulia wanajeshi mara nyingi yamekuwa yakijitokeza katika mazingira yanayohusisha kutofautiana kauli, ulevi, wivu wa kimapenzi na hata ujambazi. Hivyo katika kushughulikia hali hii, mara nyingi kesi hufunguliwa kwenye mahakama za kiraia na hukumu kutolewa kwa mujibu wa sheria zilizopo hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hakuna mtu aliye juu ya sheria inashauriwa wanaokubwa na kadhia hii wapeleke mashtaka kwa mujibu wa taratibu zilizopo ili sheria ifuate mkondo wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taratibu zilizopo za Jeshi letu la Ulinzi, afisa au askari anapopatijkana na hatia katika mahakama za kiraia na kuhukumiwa adhabu ya vifungo au nyinginezo, pia hupoteza sifa za kuendelea kulitumikia Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania. Aidha, maafisa na askari mara kwa mara wamekuwa wakiaswa kuishi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo.