Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 1 Water and Irrigation Ofisi ya Rais TAMISEMI. 4 2016-01-26

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaharakisha upatikanaji wa maji safi na salama kwa wakazi wa Kata za Manolo, Shume, Sunga na Mbaru ili kuwaondolea usumbufu Wananchi wa maeneo hayo ikiwemo ushiriki hafifu kwenye shughuli za kiuchumi?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais- TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Jimbo la Mlalo linakadiriwa kuwa na wakazi wapatao 196,258 kati yao ni asilimia 69 tu wanaopata huduma ya maji safi na salama. Aidha, kwa kutambua tatizo hilo, Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto ina mradi wa maji wa Shume, Madala na Manolo. Mradi huu unatarajiwa kugharimu jumla ya shilingi bilioni 2.96 hadi kukamilika ambapo kampuni ya Orange Contractor Ltd. kwa kushirikiana na Linda Technical Service Ltd. kutoka Mjini Lushoto na tayari mkataba umesainiwa. Hata hivyo, kazi hii inasubiri upatikanaji wa rasilimali fedha. Mradi huu unatarajia kuhudumia wananchi wapatao 33,541 katika Kata hizo. Mradi huu utakuwa na urefu wa kilomita 55, vituo 70 vya kuchotea maji pamoja na matenki matatu ya kuhifadhia maji.
Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Mbaru, Halmashauri kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Kiserikali la CHAMAVITA liliufanyia ukarabati mradi mkubwa wa maji wa Rwangi. Kwa mwaka wa fedha 2013/2014 CHAMAVITA ilitumia shilingi bilioni 96.0 kwa ajili ya kuboresha mradi huo kwa kupanua mfumo huo kutoka Kijiji cha Nkelei hadi Vijiji vya Mamboleo na Kalumele ambavyo vipo Kata ya Mbaru. Wananchi wa Vijiji hivi wanapata maji kutoka kwenye tanki la maji kwa Kwekidevu lenye ujazo wa lita 22,500.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Kata ya Sunga yenye Vijiji vitano vya Sunga, Kwemtindi, Masereka, Nkukai na Mambo inakadiriwa kuwa na wakazi wapatao 12,122. Huduma ya maji kwa Kijiji cha Mambo inapatikana kupitia visima vifupi viwili vyenye pampu ya mkono pamoja na vituo vinne vya kuchotea maji kutoka kwenye Mradi Mdogo na Mserereko ambao hauna tanki la kuhifadhia maji. Mradi huu mdogo ulijengwa na Mwekezaji wa Mambo View Hotel kwa gharama ya shilingi milioni 5.0. Katika mwaka wa fedha 2012/2013. Kwa wastani Kata ya Sunga wananchi wanaopata huduma ya maji safi na salama ni asilimia 16 tu.
Mheshimiwa Spika, vijiji vya Sunga, Kwemtindi, Masereka, Nkukai na Mambo katika Kata ya Sunga vitapewa kipaumbele mara tu baada ya vijiji kumi vya awamu ya kwanza ya programu ya maji kukamilika. Aidha, Serikali itaendelea kuboresha huduma ya maji katika Jimbo la Mlalo na maeneo mengine nchini kadri rasilimali fedha zinavyopatikana.