Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 8 Sitting 9 Enviroment Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira na Muungano 107 2017-09-15

Name

Upendo Furaha Peneza

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. UPENDO F. PENEZA aliuliza:-
Je, Serikali inatumiaje fedha za Mfuko wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabia Nchi (Adaptation Fund) zinazotolewa kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi?

Name

Dr. Susan Alphonce Kolimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI (K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS – MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Upendo Furaha Peneza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha za Mfuko wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabia nchi (Adaptation Fund AF) chini ya Mkataba wa Kimataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi zilizotolewa mwaka 2013 zinatumika kwa ajili ya kutekeleza Mradi wa Kujenga Uwezo wa Kuhimili Athari za Mabadiliko ya Tabianchi katika maeneo ya Jiji la Dar-es-Salaam. Gharama za mradi huu ni Dola za Marekani milioni tano na zinatekeleza kama ifuatavyo:-
(i) Kujenga ukuta wa bahari katika maeneo ya Barabara ya Obama (zamani Ocean Road wenye urefu wa mita 820) na Kigamboni (Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere wenye urefu wa mita 380)
(ii) Kujenga miundombinu ya mitaro ya maji ya mvua katika Mtaa wa Bungoni, Kata ya Buguruni, wenye urefu wa mita 1,003 na Mtaa wa Miburani, Kata ya Mtoni wenye urefu wa mita 800.
(iii) Kurudisha matumbawe katika ukanda wa Bahari ya Hindi, eneo la Sinda, Dar-es-Salaam lenye ukubwa wa mita za mraba 2000.
(iv) Kuendesha mafunzo kuhusu matumizi endelevu ya nishati na kusambaza majiko banifu kwa familia 3000 za Manispaa za Ilala, Temeke na Kinondoni.
(v) Kupanda mikoko katika eneo la takribani hekari 40 katika maeneo ya fukwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha za Mfuko wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi (Adaptation Fund) hutolewa kupitia njia mbili, yaani Mawakala wa Kimataifa (Multination Implementing Entities – MIEs) na Taasisi za Kitaifa (National Entities – NIEs) ambazo zimesajiliwa (accredited) na mfuko huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi unaotekelezwa katika Mkoa wa Dar-es-Salaam fedha zake zote zimetolewa kupitia katika Shirika la Umoja wa Mataifa la Hifadhi ya Mazingira (UNEP) ambaye ni Wakala wa Kimataifa. Ili kuweza kupata fedha nyingine Serikali inakamilisha sasa mchakato ambapo Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) inatarajia kusajiliwa (accredited) baada ya kukamilisha masharti yanayohitajika kuwa Taasisi ya Kitaifa ya kuratibu fedha zinazotolewa na Mfuko huu.