Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 8 Sitting 2 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 28 2017-09-06

Name

Yahaya Omary Massare

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Magharibi

Primary Question

MHE. YAHAYA O. MASSARE aliuliza:-
Shamba la Kampuni iliyokuwa ikiitwa Tanganyika Packers lenye ekari 45,000 katika Halmashauri ya Itigi limetelekezwa kwa muda mrefu na wananchi wa kata nne (4) na vijiji 12 wamekuwa wakilitumia kwa kilimo na ufugaji:-
(a) Je, ni lini Serikali itapendekeza kwa Mheshimiwa Rais kufutwa kwa hati hiyo?
(b) Je, ni lini Serikali italirudisha rasmi shamba hilo kwa Halmashauri ya Itigi ili lipangiwe matumizi kwa ajili ya wakulima na wafugaji?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yahaya Omary Massare, Mbunge wa Manyoni Magharibi, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, shamba lenye hati namba 15467 na ukubwa wa ekari 45,000 lililopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Itigi lilimilikishwa kwa Kampuni ya Tanganyika Packers Limited mwaka 1955 kwa muda wa miaka 99 kwa matumizi ya ufugaji (cattle holding).
Mheshimiwa Naibu Spika, shamba limezungukwa na Vijiji vitatu vya Kitaraka, Doroto na Kaskazi ambavyo wananchi wake kupitia uongozi wa vijiji wamekuwa wakikodishwa maeneo ya kilimo na ufugaji kutokana na shamba hilo kutoendelezwa na Mwekezaji kwa muda mrefu. Baada ya Mwekezaji kushindwa kutimiza masharti ya uendelezaji wa shamba hili, Serikali ililitaifisha shamba hili pamoja na majengo yaliyokuwa ndani yake na kuliweka chini ya uangalizi wa msajili wa Hazina. Aidha, kwa nyakati tofauti kupitia vikao vya viongozi na wananchi, Serikali imekuwa ikikataza wananchi kuvamia shamba hili kwa kuwa ni mali halali ya Serikali kwa ajili ya mipango ya uwekezaji lakini wananchi wamekuwa wakikaidi makatazo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kulifahamisha Bunge lako Tukufu kuwa, shamba hili ni mali halali ya Serikali hivyo wananchi waliovamia na kufanya maendelezo ndani ya shamba hili ni kinyume na taratibu na hivyo wasitishe shughuli zao mara moja. Serikali inaendelea kuandaa mpango wa uwekezaji utakaoleta tija ya maendeleo kwa Taifa hasa kwa wananchi wanaozunguka shamba hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali inatambua juhudi zinazofanywa na Halmashauri ya Wilaya ya Itigi katika kuleta maendeleo kwa wananchi wake. Tayari walishaleta maombi Serikalini kwa Msajili wa Hazina kwa lengo la kutaka kuingia ubia na Mwekezaji ili kuliendeleza shamba hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inayafanyia kazi maombi hayo na itatoa taarifa kamili baada ya kukamilisha tathmini ya faida na hasara zitakazotokana na uwekezaji unaopendekezwa. Natoa rai kwa viongozi wa Serikali za Vijiji na Kata kuacha kugawia wananchi eneo hilo kwa mtindo wa kuwakodisha kwa kuwa kufanya hivyo ni kinyume na taratibu za sheria ya nchi.