Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 8 Sitting 1 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 14 2017-09-05

Name

Asha Abdullah Juma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA aliuliza:-
Watanzania wengi hasa wanawake wanaokwenda kufanya kazi za ndani katika nchi za kiarabu kama Oman na nyinginezo wamekuwa wakifanyiwa ukatili mkubwa sana unaosababisha wengine kufariki na wengine kujeruhiwa vikali.
(a) Je, Serikali ina utaratibu gani madhubuti wa kudhibiti safari za Watanzania hao wanaokwenda katika nchi za Kiarabu na pia kuwabana Mawakala na kuwawajibisha inapobidi?
(b)Je, ni wanawake wangapi wa Kitanzania wameuawa katika Nchi za Kiarabu na fidia kutolewa katika familia zao?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka utaratibu mzuri wa kutoa vibali kupitia mamlaka zinazoshughulikia masuala ya ajira ikiwemo Wakala wa Huduma za Ajira Tanzania (TAESA) iliyopo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia masuala ya kazi, vijana, ajira na watu wenye ulemavu kwa kushirikiana na Wizara inayoshugulikia masuala ya kazi Zanzibar na Balozi zetu zilizoko nchi mbalimbali huko Mashariki ya Kati.
Serikali imeweka miongozo itakayosaidia siyo tu kuwabana mawakala bali pia kuwasaidia Watanzania kutumia fursa za ajira zilizopo nje ya nchi ili kupunguza tatizo la ajira hasa kwa vijana kwa kuelekeza kila mfanyakazi kuwa na wakala rasmi na kupata mkataba kutoka Ubalozini.
Mheshimiwa Spika, Ubalozi unakuwa na taarifa katika kila hatua ambayo Watanzania wanapitia wakati wa maandalizi ya kwenda kufanya kazi hivyo kulinda maslahi yao. Aidha, mwajiri anayetaka kuajiri wafanyakazi kutoka Tanzania atatakiwa kusoma na kuelewa mwongozo na baada ya kukubaliana nao anatakiwa kujaza fomu ya kuomba kumwajiri Mtanzania na kuwasilisha Ubalozini kwa ajili ya kufanyiwa kazi. Maombi hayo yatafuatiwa na mkataba wa kazi.
Mheshimiwa Spika, mkataba huu una vupengele vikuu vitano ambavyo mwajiri na mawakala wanapaswa kukidhi mahitaji yake ili Serikali itoe idhini kwa Mtanzania aliye tayari kufanya kazi aendelee na taratibu za ajira katika nchi hizo. Vipengele hivyo ni kama ifuatavyo:-
(i) Taarifa za mwajiri.
(ii) Taarifa za mwajiriwa.
(iii) Mshahra wa mwajiriwa.
(iv) Masharti ya mkataba.
(v) Maelezo ya mawakala wa Tanzania na Oman.
Mheshimiwa Spika, takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa Watanzania zaidi ya 12,000 ambao Balozi unawatambua wanafanya kazi katika kada mbalimbali nchini Oman. Kati ya hao, wanawake watatu wamepoteza maisha kwa sababu mbalimbali ikiwemo ugonjwa, ajali na kadhalika. Katika vifo vilivyowahi kuripotiwa ambapo Serikali ilifuatilia hadi kujua vyanzo halisi vya vifo hivyo, hakuna taarifa kuhusu vifo vilivyosababishwa na mauaji ya makusudi.
Aidha, mara zote tunapopata taarifa za vifo katika nchi hizo, Serikali huchukua jukumu la kufuatilia kwa kushirikiana na mamlaka za nchi husika kujua hatma za familia zilizopoteza mwenzi wao ikiwa ni pamoja na malipo ya fidia kutoka kwa mwajiri wa marehemu.
Mheshimiwa Spika, wakati wote Serikali imekuwa makini katika hatua za awali za maandalizi ya safari hizo kwa kuwabana mawakala na kuhakikisha kuwa mikataba inakuwa ni mizuri ili kuwezesha kuziba mianya yote ya kukwepa majukumu kwa pande zote inayoweza kusababisha Watanzania wanaokwenda kufanya kazi katika nchi hizo kupoteza haki zao.