Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 29 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 243 2017-05-19

Name

Ussi Salum Pondeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chumbuni

Primary Question

MHE. USSI SALUM PONDEZA aliuliza:-
Askari Polisi Zanzibar kwa muda mrefu wamekuwa wakilazimika kutumia fedha zao za mfukoni kuwahudumia chakula mahabusu wanoshikiliwa katika Vituo vya Polisi Unguja wakati jukumu hilo ni la Serikali.
(a) Je, Serikali imechukua hatua gani za kuondoa tatizo hilo tangu kulalamikiwa na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora baada ya kufanya ziara ya ukaguzi na kugundua tatizo hilo?
(b) Je, ni sababu gani zimepelekea chakula kutopelekwa katika Vituo vya Polisi wakati Bunge limekuwa likiridhia matumizi ya Wizara kila mwaka zikiwemo gharama za chakula kwa mahabusu?
(c) Je, haki za binadamu zinazingatiwa vipi inapotokea askari hawana fedha za kununua chakula cha mahabusu na kulazimika kulala na njaa wakati Serikali ndiyo yenye jukumu la kuwapatia huduma ya chakula?

Name

Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ussi Pondeza, kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, mahabusu wanaoshikiliwa katika Vituo ya Polisi huhudumiwa na Jeshi la Polisi kwa kuwapatia mahitaji muhimu kama chakula na malazi. Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikitenga bajeti kwa ajili ya chakula cha mahabusu kwa kila mwaka.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, si kweli kwamba chakula huwa hakipelekwi katika mahabusu za polisi. Chakula hupelekwa kulingana na idadi ya mahabusu kama ambavyo taratibu za utoaji wa chakula zinavyoelekeza katika PGO 356.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, kulisha mahabusu walioko katika Vituo ya Polisi ni jukumu la Serikali na si askari mmoja mmoja kutumia fedha zake za mfukoni kwa kufanya jukumu hilo. Serikali itaendelea kutimiza wajibu huo na hakuna uvunjaji wa haki za binadamu katika kuwapatia huduma za chakula mahabusu.