Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 29 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 242 2017-05-19

Name

Devotha Methew Minja

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA M. MINJA aliuliza:-
Waandishi wa Habari wanafanya kazi nzuri katika kuelimisha jamii.
Je, ni lini Serikali itaanzisha mfumo utakaotambua kazi zinazofanywa na tasnia ya habari?

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kujibu swali hili, naomba uniruhusu nianze kwa kuipongeza timu yetu ya vijana ya Serengeti kwa ushindi wa mabao mbili kwa moja dhidi ya Angola jana nchini Gabon. (Makofi)
Vilevile nichukue nafasi hii kuwapongeza Watanzania wote kwa kushikamana na kushirikiana pamoja kuichangia na kuishangilia pamoja na kuitakia kheri timu yetu hii ya vijana ya Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huu mfupi, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Minja, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua na kuthamini kazi zinazofanywa na vyombo vya habari nchini. Mchango wa tasnia ya habari ni mkubwa katika kuhabarisha, kuelimisha na kuburudisha jamii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua mchango huo, Serikali imeruhusu uwepo wa vyombo vya habari vya umma na sekta binafsi, yakiwemo makampuni binafsi, mashirika ya kidini na kijamii. Aidha, mchango wa vyombo vya habari unatokana na sera, sheria, mipango na taratibu zilizowekwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo unaotambua kazi za tasnia ya habari nchini upo tayari. Katika kudhihirisha hilo, Serikali ilitunga Sera ya Habari na Utangazaji ya mwaka 2003, Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976 na sasa ina Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya mwaka 2016 na Kanuni zake za mwaka 2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuweka mazingira mazuri ya kuwezesha wanahabari kufanya kazi zao kwa weledi na kwa kuzingatia kanuni, sheria na taratibu ili kulinda amani na utulivu katika nchi yetu. Wizara yangu kwa sasa inaainisha mahitaji ya wataalamu katika tasnia ya habari ili kushirikiana na wadau wa ndani na nje tuweze kuwapatia mafunzo kwa lengo la kuboresha kazi zao.