Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 29 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 241 2017-05-19

Name

Alex Raphael Gashaza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngara

Primary Question

MHE. ALEX R. GASHAZA aliuliza:-
Maporomoko ya maji ya Rusumo yanapatikana katika Jimbo la Ngara nchini Tanzania na Wilaya ya Kirehe nchini Rwanda kwenye mpaka wa Tanzania na Rwanda na maporomoko haya yanaweza kuwa kivutio kizuri cha kitalii.
Je, Serikali iko tayari kufanya utafiti katika eneo hili ili liweze kurasimishwa kwa ajili ya shughuli za kitalii ili kuongeza pato la Wilaya na Taifa kupitia sekta hiyo ya utalii?

Name

Prof. Jumanne Abdallah Maghembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwanga

Answer

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Alex Raphael Gashaza, Mbunge wa Ngara, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa maporomoko ya maji ya Rusumo yaliyopo Wilayani Ngara, Mkoa wa Kagera, yana uwezo wa kuwa kivutio kizuri cha utalii katika Kanda ya Ziwa Victoria. Wizara iliwahi kutembelea eneo hilo na kushauri kuwa linaweza kutembelewa kama kivutio. Maeneo mengine yanayoweza kujumuishwa katika maporomoko hayo kama kivutio ni maeneo ya hifadhi za Burigi na Kimisi, Bioanuwai ya pekee katika katika misitu ya asili ya Minziro, mapango ya watumwa katika Kata ya Kenza na maporomoko ya maji katika Msitu wa Rubare pamoja na maji ya moto katika Msitu wa Mutagata.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara iko tayari kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Ngara kufanya utafiti unaoweza kuendeleza na kurasimisha maporomoko hayo na mandhari yake kuwa kivutio cha utalii kitakachoongeza pato la Wilaya na Taifa kwa ujumla.