Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 27 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 221 2017-05-17

Name

Riziki Shahari Mngwali

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RIZIKI S. MNGWALI aliuliza:-
(a) Je, Serikali ina utaratibu gani maalum wa kuwapangia na kuwahamisha sehemu za kazi watumishi wake?
(b) Je, ni vigezo gani huzingatiwa katika kuwapanga au kuwahamisha watumishi sehemu za kazi?
(c) Je, ni kwa namna gani Serikali inahakikisha watumishi wake wanafanya kazi kwa ufanisi katika maeneo waliyopangwa?

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Riziki Shahari Mngwali, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ukiacha watumishi wa kada ya ualimu na wale wa kada za afya ambao utaratibu wao wa kuajiriwa ni wa kupangiwa vituo vya kazi mara tu wanapohitimu mafunzo yao, utaratibu wa ajira kwa kada nyingine hufanyika kwa mujibu wa Sheria ya Utumishi wa Umma Namba 8 ya mwaka 2002.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa sheria hii, mchakato wa ajira hufanywa na Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma ambayo hutangaza kazi kulingana na mahitaji ya waajiri, kufanya usaili na kuwapeleka katika vituo vya kazi waombaji waliofaulu usaili.
Mheshimiwa Naibu Spika, uhamisho ndani ya utumishi wa umma hufanywa kwa mujibu wa Sheria ya Utumishi wa Umma, Sura 298 ikisomwa kwa pamoja na Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma, Toleo la mwaka 2009 ambapo Katibu Mkuu (Utumishi) amepewa mamlaka ya kufanya uhamisho wa watumishi wa umma kutoka kwa mwajiri mmoja na kwenda kwa mwingine kwa lengo la kuimarisha utendaji ndani ya Utumishi wa Umma.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, vigezo vinavyotumika kuwapanga au kuwahamisha vituo vya kazi watumishi wa umma ni pamoja na:-
(i) Mahitaji ya kila taasisi kutokana na kuwepo ikama na bajeti ya mishahara ya watumishi kwa mwaka wa fedha husika.
(ii) Sifa za kitaaluma kama zilivyoainishwa kwenye Miundo ya Maendeleo ya Utumishi kama inavyotolewa mara kwa mara na Serikali.
(iii) Umuhimu wa kuimarisha utendaji wa kazi na kuongeza ufanisi katika utumishi wa umma.
(iv) Kupangiwa kazi au uhamisho kutokana na mtumishi kupata maarifa/taaluma mpya (re-categorization).
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha watumishi wanafanya kazi kwa ufanisi katika maeneo waliyopangwa, zipo Mamlaka za Ajira na Nidhamu ambazo zimewekwa kwa mujibu wa Sheria ya Utumishi wa Umma Sura 298. Kwa mujibu wa sheria hii, mamlaka hizi zinapaswa kuhakikisha kuwa kila mtumishi anapangiwa majukumu kulingana na mpango mkakati wa kila taasisi, ambapo kila mwisho wa mwaka upimaji wa wazi wa utendaji kazi hufanyika. Pale mtumishi anapoonekana hajatimiza malengo yake kwa sababu yoyote ile, anapaswa kuchukuliwa hatua stahiki kwa mujibu wa sheria na kanuni zinazoongoza usimamizi wa utumishi wa umma.