Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 19 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 160 2017-05-08

Name

Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza:-
Kumekuwa na ujenzi wa nyumba za ghorofa kando kando ya barabara kuu na Serikali ndiyo inatoa vibali vya ujenzi huu ambapo baada ya muda maghorofa hayo yanaweza kubomolewa na mwenye jengo kulipwa fidia.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuainisha maeneo yenye mipango ya maendeleo ili kuepuka gharama kubwa ya kulipa fidia?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MANDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Nassoro Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na ujenzi wa nyumba za ghorofa na za kawaida kando kando ya barabara kuu na barabara nyingine. Kasi ya ujenzi wa nyumba hizo huchochewa na kuimarika kwa miundombinu hususan barabara za kiwango cha lami. Uimarishaji wa barabara za lami huvutia wawekezaji kujenga nyumba za biashara, vituo vya mafuta, mahoteli pamoja na makazi. Hali hii ni ya kawaida katika uendelezaji miji kwa kuwa uboreshaji miundombinu hususan barabara hupandisha thamani ya ardhi katika eneo husika na kuvutia ujenzi wa majengo ya ghorofa.
Mheshimiwa Spika, ili kupunguza uwezekano wa kubomoa au kulipa fidia maeneo yaliyoendelezwa kwa ujenzi wa nyumba za ghorofa, Serikali imejiwekea mikakati ifuatayo:-
(i) Kuanisha meneo yote ambayo yameiva kiundelezaji upya (areas ripe for redevelopment) ili kuoanisha matumizi ya sasa na ya baadaye.
(ii) Kupanga maeneo hayo ili uendelezaji wake uendane na thamani ya ardhi na kuboresha sura ya miji. Mipango kina ya uendelezaji maeneo haya ni kama vile Kariakoo, Kurasini, Temeke, Msasani, Oysterbay, Magomeni na Ilala.
(iii) Kwa upande wa miji mingine, upangaji wa maeneo haya unazingatiwa katika utayarishaji wa mipngo kabambe (master plan) ya miji husika.
Mheshimiwa Spika, ujenzi wa nyumba za ghorofa kando ya barabara kuu hauna budi kufuata taratibu za mipango miji, uhandisi, mazingira na masharti ambayo muendelezaji hupewa katika kibali chake cha ujenzi. Natoa rai kwa taasisi zenye mamlaka ya kutoa vibali vya ujenzi ambazo ni Halmashauri za Wilaya, Miji, Manispaa pamoja na Majiji kuzingatia masharti ya uendelezaji wa miji ili kuzuia uwezekano wa kubomoa maghorofa na kulipa fidia.