Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 15 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 122 2017-05-02

Name

Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HAWA A. GHASIA (K.n.y. MHE. AMINA N. MAKILAGI) aliuliza:-
Je, Serikali ina mikakati gani ya kupima ardhi yote ya Tanzania na kuipangia matumizi yaliyo bora kufuatia kuwepo kwa tatizo kubwa la migogoro ya ardhi kati ya wakulima, wafugaji na Mamlaka ya Hifadhi?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Nassoro Makilagi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni azma ya Serikali kuondoa migogoro ya ardhi kote nchini na ili kufikia azma hiyo, Serikali imeandaa programu ya kupanga, kupima na kumilikisha kila kipande cha ardhi nchini.
Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa programu
hii, kila kipande cha ardhi nchini kitapangiwa matumizi na kupimwa, hali ambayo itaondoa mwingiliano baina ya watumiaji mbalimbali wa ardhi na hivyo kupunguza uwezekano wa kuibuka kwa migogoro ya ardhi. Mpango huu utasaidia ardhi yote kutunzwa na watumiaji husika na kuhifadhi maliasili zilizopo katika mazingira kwa ujumla.
Mheshimiwa Spika, pia jamii inayozunguka maeneo
hayo yaliyohifadhiwa itawezeshwa kutambua mipaka yao na kuwa na mipango ya matumizi ya ardhi na kudhibiti uvamizi wa maeneo ya hifadhi. Aidha, utekelezaji wa programu hii utajenga uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa kulinda ardhi inayomilikiwa dhidi ya uvamizi wowote, kuwezesha kukabliana na athari zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi, kuboresha makazi ya wananchi na kuleta usalama na ustawi wa maliasili za Taifa.
Mheshimiwa Spika, programu ya kupanga, kupima
na kumilikisha kila kipande cha ardhi nchini itahusisha Halmashauri zote 181 nchini na imepangwa kufanyika katika kipindi cha miaka kumi kwa awamu ya miaka mitano kwa kila awamu kuanzia mwaka wa fedha 2016/2017.
Aidha, programu hii itakuwa na miradi mikubwa miwili ambayo ni miradi ya upimaji wa kila kipande cha ardhi vijijini na mradi wa upimaji wa kila kipande cha ardhi mijini.
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa programu hii kwa awamu ya kwanza, umeanza kupitia Mradi wa Land Tenure Support Program ambao unatekelezwa katika Wilaya tatu za mfano katika Wilaya za Kilombero, Malinyi na Ulanga ambayo hadi sasa jumla ya mipaka ya vijiji 50 imeshapimwa na kazi ya uandaaji wa mpango wa matumizi bora ya ardhi, upimaji wa vipande vya ardhi na utoaji wa hatimiliki za kimila, unaendelea.