Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 12 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 95 2017-04-25

Name

Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE.OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Ibara ya 57(b) ya Ilani ya CCM inaahidi kuweka mfumo wa kuvitambua, kuvisajili na kuviwezesha vikundi vyote vyenye mwelekeo wa ushirika na ujasiriamali nchini. Kwa kuwa kundi la waendeshaji wa vyombo vya usafiri wa abiria maarufu kama bodaboda ni kundi la kijasiriamali, na inawezekana ndilo kundi lenye mwelekeo na fursa za kiushirika ambalo ni kubwa zaidi Wilayani Biharamulo na nchini kote kwa sasa.
Je, Serikali ina mpango gani mahususi juu ya kundi hili?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha Ibara ya 57(b) ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 inatekelezwa kikamilifu kuhusu uwezeshaji, Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo imeweza kuvitambua na kuvisajili jumla ya vikundi 1,940 vya wajasiriamali vikiwemo vikundi 34 vya vijana waendesha bodaboda. Aidha, waendesha bodaboda 2,000 wametambuliwa kwa jitihada kubwa za Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na Halmashauri na wakawekewa utaratibu wa utoaji huduma ya usafiri wa pikipiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi Wilaya ya Biharamulo imewezesha jumla ya waendesha bodaboda 410 kupata mafunzo ya uendeshaji wa pikipiki na kupata leseni za kuendesha na kufanya biashara hiyo.
Natoa wito kwa Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhamasisha waendesha bodaboda wajiunge kwenye vikundi na SACCOS ili watambulike kisheria na kupata fursa ya mikopo inayotolewa kupitia asilimia 10 ya vijana na wanawake pamoja na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Kiuchumi.