Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 11 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 87 2017-04-24

Name

Muhammed Amour Muhammed

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Bumbwini

Primary Question

MHE. SALEH ALLY SALEH (K.n.y. MUHAMMED AMOUR MUHAMMED) Aliuliza:- Kwa kipindi kirefu sasa kumekuwa na matendo ya dhahiri yanayoonesha kuvunjwa kwa haki za binadamu hapa nchini bila ya Serikali kuchukua hatua yoyote.
Je, Serikali haioni kwamba wananchi watakosa imani na Serikali yao?

Name

Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Answer

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA Alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Muhammed Amour Muhammed, Mbunge wa Bumbwini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya jukumu la msingi kwa Serikali ni kukuza, kulinda na kuhifadhi haki za binadamu na wajibu wao hapa nchini. Jukumu hilo ni la kikatiba ambapo Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, kama ilivyorekebishwa mara kwa mara na Katiba ya Zanzibar ya 1984 kama ilivyorekebishwa mara kwa mara pamoja na kuainisha haki za binadamu, imeipa Serikali wajibu wa kukuza, kulinda na kuhifadhi haki hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kupitia Bunge lako Tukufu, nchi yetu imeridhia mikataba mbalimbali ya Kimataifa na kikanda ambayo inaweka misingi ya haki hizo na wajibu wa Serikali katika kuhakikisha nchi inaendeshwa kwa kufuata misingi ya haki za binadamu. Aidha, Bunge lako Tukufu kwa nyakati tofauti limetunga sheria mbalimbali zinazolinda na kukuza haki za binadamu pamoja na kutoa nafuu (remedy) kwa raia pale haki za binadamu zinapovunjwaaidha na Serikali au mtu binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha haki za binadamu zinalindwa, zinadumishwa na zinastawishwa hapa nchini, Katiba imeipa Mahakama mamlaka ya kusikiliza na kuamua mashauri yanayohusu haki za binadamu na wajibu wao kama ulivyoainishwa katika Katiba. Aidha, Serikali imeunda taasisi mbalimbali zinazoshughulikia hifadhi ya haki za binadamu. Taasisi hizo ni pamoja na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma na Mabaraza mbalimbali kama yale ya Ardhi na Kodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama pamoja na taasisi hizi zimekuwa zikichukua hatua pindi vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu vinapotokea na kuripotiwa au kufikishwa kwa maamuzi. Serikali kupitia vyombo vyake, imejidhatiti kuhakikisha kuwa kitendo chochote kinachovunja haki za binadamu kinachukulia hatua stahiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwasihi Waheshimiwa Wabunge tushirikiane na vyombo vyetu vilivyopewa mamlaka na dhamana ya kulinda haki pale tunapopata taarifa za vitendo vya uvunjwaji wa haki za binadamu vimefanyika au vinaweza kufanyika ili hatua stahikina za haraka za kisheria zichukuliwe.