Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 9 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 72 2017-04-19

Name

Savelina Slivanus Mwijage

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SAVELINA S. MWIJAGE Aliuliza:-
Nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) ni za muda mrefu na zimekuwa chakavu sana na nyingine zimeanza kubomoka.
(a) Je, ni lini Serikali itafanya operesheni kubaini uharibifu ulioko kwenye nyumba hizo?
(b) Je, ni lini Serikali itatenga bajeti kwa ajili ya kukarabati au kujenga upya nyumba hizo?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Savelina Silvanus Mwijage, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifutavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) ambazo ni za muda mrefu na kati ya hizo zipo zilizo katika hali chakavu ambazo idadi yake si kubwa sana ukilinganisha na nyumba zilizo katika hali nzuri kimatengenezo. Ili kuhakikisha nyumba zote zinakuwa katika hali nzuri na bora kimatengenezo, Shirika limeweka mpango mkakati wa kuhakikisha kwamba nyumba zote zilizo katika hali ya uchakavu zinafanyiwa ukarabati mkubwa na kwa nyumba ambazo kiwango cha ukachakavu ni kikubwa sana (beyond repair) shirika limeweka utaratibu wa kuzivunja na kuendeleza upya viwanja hivyo kwa kujenga majengo ya kisasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Nyumba la Taifa limefanya uhakiki wa nyumba zake zote na kubaini hali halisi ya kila nyumba na kuweka mpango wa kuzifanyia ukarabati nyumba hizo kwa awamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2016/2017 shirika lilitenga takriban shilingi bilioni 11, kwa ajili ya kuzifanyia ukarabati nyumba zake ambapo hadi Machi, 2017 jumla ya nyumba 2,451 zilikuwa zimekwishafanyiwa ukarabati mkubwa kupitia bajeti hiyo. Aidha, idadi ya nyumba zilizofanyiwa ukarabati mkubwa inatarajiwa kuongezeka ifikapo mwisho wa mwezi Juni, 2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, shirika linatarajia kumaliza kuzifanyia ukarabati nyumba zote katika Mwaka wa Fedha 2017/2018. Hata hivyo, ni vema ikafahamika kuwa matengenezo ya nyumba ni kazi endelevu kwa shirika, hivyo bajeti ya matengenezo itaendelea kutengwa kila mwaka ili wapangaji wa nyumba za shirika waendelee kuishi katika nyumba na mazingira bora.