Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 7 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 56 2017-04-13

Name

Salma Mohamed Mwassa

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SALMA M. MWASSA aliuliza:-
Je, ni nini umuhimu wa kurasimisha ardhi kwenye maeneo ambayo hayajapimwa?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salma Mohamed Mwassa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, urasimishaji wa ardhi maana yake ni kutambua miliki za wananchi kwenye maeneo yaliyoendelezwa bila kupimwa kisheria. Matokeo ya urasimishaji ni kutoa hatimiliki na kuweka miundombinu ya msingi kama vile barabara, maji, mifereji ya maji ya mvua na
ikiwezekana kuweka majina ya mitaa. Kwa kawaida, urasimishaji ni zoezi shirikishi limalowezesha wananchi kukubaliana mipaka ya viwanja, kufungua njia na kutoa maeneo ya huduma za jamii kama vile shule, vituo vidogo vya polisi, makaburi, zahanati na maeneo ya wazi.
Mheshimiwa Spika, umuhimu wa kurasimisha maeneo haya ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, la kwanza, urasimishaji unatoa fursa kwa wananchi kutumia ardhi kupitia nyaraka za umiliki wa ardhi kama vile hati, kuweka dhamana ya mikopo katika taasisi za fedha, mahakama.
Mheshimiwa Spika, la pili ni kuongeza thamani ya ardhi au nyumba husika (value addition) iwe kwa kuweka dhamana (collateral) rehani, upangishaji na kadhalika.
Mheshimiwa Spika, tatu ni kuboresha makazi hususan kwa kuweka miundombinu ya msingi ili kurahisisha usafiri, kupunguza madhara yatokanayo na majanga mbalimbali kama vile mafuriko na moto. Kwa upana wake urasimishaji ni dhana inayochangia kupunguza umaskini.
Mheshimiwa Spika, nne ni kutoa uhakika wa milki ya ardhi na hivyo kuwa kivutio kwa mazingira ya uwekezaji. Kwa mfano, maeneo mengi ambayo yamerasimishwa, kumekuwa na uwekezaji wa shughuli za kiuchumi kama vile mahoteli, maduka, shule, hospital na maeneo ya burudani na kadhalika Mheshimiwa Spika, tano vilevile ni kupunguza migogoro ya ardhi.
Mheshimiwa Spika, napenda kusisitiza kuwa, urasimishaji si jibu la kudumu la kuzuia ujenzi holela mijini bali ni utayarishaji wa mipango kabambe ya miji yetu ambayo ikienda sambamba na uimarishaji wa usimamizi na uthibiti wa uendelezaji miji itaweka ustawi mzuri wa mandhari ya nchi yetu na hivyo kufanya nchi yetu kuwa sehemu nzuri ya kuishi.