Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 4 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 32 2017-04-10

Name

Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Primary Question

MHE. JANET Z. MBENE aliuliza:-
Jumuiya za kiuchumi za Kikanda zimekuwa sehemu ya mkakati mkubwa katika kuratibu masuala ya kiuchumi, kijamii, kisiasa na kimazingira. Ileje ni Wilaya ya mpakani mwa Nchi za Malawi na Zambia lakini haina kituo cha forodha. Hakuna miundombinu ya soko la Kimataifa, hakuna kituo cha uhamiaji, hakuna kituo cha kudhibiti mazao, mifugo wala silaha. Hii inasababisha wahamiaji haramu na wahalifu kutumia mipaka kinyume cha sheria na taratibu:-
Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha forodha, kituo cha uhamiaji, soko la Kimataifa na kituo cha kukagua mifugo na silaha kwa ufanisi na maendeleo ya Ileje?

Name

Dr. Philip Isdor Mpango

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene, Mbunge wa Ileje kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli kabisa kuwa katika Wilaya ya Ileje hakuna kituo cha forodha na uhamiaji wala soko la Kimataifa na vituo vya kukagua mifugo na silaha. Namshukuru sana Mheshimiwa Mbunge ambaye ameendelea kufuatilia jambo hili kwa nguvu sana na kwa kutambua umuhimu huo, Mamlaka ya Mapato na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi tayari tumefanya jitihada tumepata kiwanja kwa ajili hiyo lakini bado tunafanya mashauriano na nchi jirani na hususani Zambia na Malawi kwa sababu ya utaratibu wa kujenga kituo cha pamoja lakini pia tutahitaji maandalizi kwa ajili ya kuamua jengo lenyewe hilo la kituo cha pamoja liweje.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kazi hizo kukamilika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaanza utekelezaji wa ujenzi wa kituo hicho mara baada ya kuwa shughuli hiyo imekamilika, lakini kwa sasa natoa rai kwa niaba ya Serikali kwa wananchi wa Wilaya ya Ileje na Wilaya zinazofanana na hizo kuendelea kutumia huduma zilizo katika Wilaya na Mikoa jirani wakati tunafanya utaratibu wa kujenga vituo hivyo.