Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 4 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 31 2017-04-10

Name

Desderius John Mipata

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkasi Kusini

Primary Question

MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Hapa nchini pamekuwepo na ongezeko kubwa la Taasisi mbalimbali zinazotoa huduma za kifedha kama vile Benki, Vikundi mbalimbali kama VICOBA, Taasisi za Kukopesha Watumishi, Taasisi za kukopesha wafanyabiashara na wakati mwingine watu na mitaji yao wanakopesha watumishi (kienyeji) kwa kificho ficho:-
(a) Je, ni chombo kipi hasa chenye wajibu wa kufuatia kodi zinazotozwa na wananchi?
(b) Je, kodi zinazotozwa ni halali?
(c) Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha wananchi
wake hawaibiwi kwa njia hiyo?

Name

Dr. Philip Isdor Mpango

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la
Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini,
kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977, Toleo la 2005, Ibara ya 138(1) inaelekeza kuwa, hakuna kodi ya aina yoyote itakayotozwa isipokuwa kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Bunge au kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa Kisheria na uliotiwa nguvu Kisheria na Sheria iliyotungwa na Bunge
Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Mamlaka ya Mapato Tanzania, Sura ya 399(5) imeipatia Mamlaka ya mapato wajibu wa kukadiria, kutoza na kutoa hesabu za mapato yote ya umma. Aidha, Sheria ya bajeti kifungu cha 58(b) inaelekeza kuwa mtu yeyote aliyepewa Mamlaka ya kukusanya mapato ya Serikali atawajibika kukusanya kwa ufanisi, kutoa hesabu za mapato, kuyawasilisha na kuyatolea taarifa kwa kuzingatia Sheria husika na kuchukua tahadhari kuzuia usimamizi mbovu wa mapato na pale inapolazimu, mfano; katika operesheni maalum dhidi ya wakwepa kodi sugu au mazingira hatarishi, TRA inaweza kuomba msaada wa vyombo vingine vya dola.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kodi halali zinazotozwa kwenye huduma za kifedha kwa mujibu wa Sheria ni zifuatazo:- Kodi ya zuio kwenye faida inayolipwa kwa Mwekezaji ambayo ni pamoja na amana za Benki, dhamana za Makampuni au Serikali na hisa; Kodi za ongezeko la thamani kwenye ada zinazotozwa kwenye huduma za kifedha na ushuru wa bidhaa kwenye ada inayotolewa kwenye kutuma au kupokea fedha kwa njia za kielektroniki na hususani simu za mkononi.
Mheshimiwa Naibu Spika, endapo mtu binafsi ama
Taasisi itatoza ama kukusanya kodi yoyote kinyume na matakwa ya Sheria, anakuwa ametenda kosa na hatua stahiki zinapaswa kuchukuliwa mara moja dhidi yake.