Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 1 Public Service Management Ofisi ya Rais TAMISEMI. 01 2017-04-04

Name

Khalifa Mohammed Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Mtambwe

Primary Question

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA aliuliza:-
Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) upo katika Awamu ya Tatu ya utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ili ziweze kumudu mahitaji ya chakula, elimu, afya na lishe bora kwa watoto:-
(a) Je, Serikali haioni ipo haja ya kuongeza viwango vya ulipaji kwa kaya maskini hasa ukizingatia upandaji wa bei za mahitaji ya kila siku na kuporomoka kwa thamani ya sarafu yetu?
(b) Je, ni vigezo gani vya uhakika vinatumika ili kupata kaya maskini?

Name

George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Khalifa Mohamed Issa, Mbunge wa Jimbo la Mtambwe, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ni wa miaka kumi na utatekelezwa kwa vipindi viwili vya miaka mitano mitano kuanzia mwaka 2013 – 2023. Madhumuni ya Mpango huu ni kuwezesha kaya maskini kuongeza kipato na fursa na kuinua kiwango cha matumizi yao.
Mheshimiwa Spika, kiwango kinachotolewa kwa walengwa ni ruzuku ambayo ni kichocheo cha kuifanya kaya iweze kujikimu hasa katika kupata mahitaji muhimu huku ikiendelea kujiimarisha kiuchumi kwa kuweka akiba na kutekeleza miradi ya ujasiriamali ili iweze kusimama yenyewe na kujitegemea baada ya kutoka kwenye umaskini uliokithiri.
Mheshimiwa Spika, ruzuku inayotolewa kwa walengwa imeongezwa baada ya kufanyiwa mapitio kwa kuangalia hali halisi. Hata hivyo, ieleweke kwamba viwango vinavyotolewa vilipangwa hivyo ili kaya maskini iendelee kujishughulisha na kazi nyingine za kuongeza kipato na
isitegemee ruzuku peke yake. Kwa uzoefu uliopatikana, umeonesha kwamba kwa kiwango hicho walengwa wameweza kuboresha maisha yao kwa kufanya shughuli mbalimbali ikiwemo kilimo, ufugaji, ujasiriamali na ujenzi wa nyumba bora, hivyo viwango hivyo vya ruzuku sio kidogo kama wengi wetu tunavyodhani.

(b) Mheshimiwa Spika, vigezo vya kupata kaya maskini huainishwa na jamii katika mkutano wa hadhara unaoendeshwa na wawezeshaji kutoka Halmashauri za Wilaya na kusimamiwa na viongozi wa vijiji/mitaa/shehia. Jamii huweka vigezo vya kaya maskini sana katika maeneo
yao. Hata hivyo, vigezo vikuu katika maeneo mengi ni kaya kukosa/kushindwa kugharamia mlo mmoja kwa siku, kaya kuwa na watoto ambao hawapati huduma za msingi kama elimu na afya kutokana na kuishi katika hali duni, wazee, wagonjwa wa muda mrefu na watoto yatima wanaoishi katika mazingira magumu na pia kukosa makazi ya kudumu au nyumba na mavazi muhimu.