Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 4 Public Service Management Ofisi ya Rais TAMISEMI. 45 2017-02-03

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Primary Question

MHE. JAPHET N HASUNGA aliuliza:-
Kwa kuwa watumishi na viongozi wengi wamekuwa wanaingia kwenye madaraka mbalimbali ya nchi bila kupewa mafunzo ya kuwaandaa kama ilivyo katika nchi nyingi duniani na kama ilivyo kwenye vyombo vya majeshi yetu.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa viongozi wote wanapewa mafunzo ya awali kabla ya uteuzi wa madaraka yoyote katika utumishi wa umma?

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Japhet Ngailonga Hasunga, Mbunge wa Jimbo la Vwawa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuwapatia mafunzo ya awali watumishi na viongozi wa umma kabla ya uteuzi wa madaraka yoyote katika utumishi wa umma ili waweze kuuelewa utumishi wa umma na kufahamu misingi yake, sheria, kanuni na taratibu za utendaji kazi na kuwapatia stadi za uongozi zinazowezesha kutekeleza majukumu yao kwa weledi na ufanisi. Katika kutekeleza azma hii Serikali imechukua hatua zifuatazo:-
(a) Imeandaa na kuendesha mafunzo elekezi kwa watumishi wanaoteuliwa kushika nafasi za uongozi ili waweze kumudu madaraka mapya.
(b) Imeendelea kutoa mafunzo ya uongozi (Leadership Development Programmes), kwa watumishi waandamizi kwa lengo la kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, lakini pia kuwaandaa kwa ajili ya kushika nafasi za uongozi pindi watakapoteuliwa kushika nafasi hizo. Mafunzo hayo yamekuwa yakiendeshwa na taasisi mbalimbali za Serikali ikiwemo Taasisi ya Uongozi, Wakala wa Mafunzo kwa njia ya Mtandao (TaGLA), Chuo Kikuu cha Mzumbe pamoja na ESAMI. Katika kipindi cha mwaka 2015/2016 watumishi waandamizi 1,397 waliweza kupatiwa mafunzo ya uongozi.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kupitia Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Serikali imeanzisha Chuo cha Taifa cha Ulinzi (National Defence College of Tanzania) kinachotoa mafunzo ya uongozi kwa Maafisa Waandamizi wa Kijeshi na Kiraia (Inter Service Training) kwa kuhusisha Maafisa wa Jeshi na wa Kiraia (Defence-Civil Staff Training) ikiwa ni pamoja na kuwapatia uelewa wa masuala ya usalama na hivyo kuwajengea uwezo wa kutambua athari za kiusalama wanapotunga na kutekeleza sera, sheria na maamuzi mbalimbali ya kiutendaji.
(d) Mheshimiwa Mweenyekiti, lakini pia, Serikali kupitia Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kimetoa mafunzo kwa viongozi waandamizi 86 na kiko katika maandalizi ya kuandaa utaratibu wa kuwa na mafunzo ya lazima kwa Maafisa Waandamizi katika utumishi wa umma (Mandatory Course for Senior Officers in the Public Service). Mafunzo haya ya lazima yanalenga kuwawezesha Maafisa Waandamizi kujua majukumu ya msingi ya uongozi na usimamizi katika taasisi za umma, hivyo kuwaandaa na kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu hayo pindi watakapoteuliwa kushika nafasi za uongozi.