Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 4 Education, Science,Technology and Vocational Training, Ofisi ya Rais TAMISEMI. 43 2017-02-03

Name

Vedastus Mathayo Manyinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Musoma Mjini

Primary Question

MHE.VEDASTUS M. MANYINYI aliuliza:-
Baada ya Serikali kutoa tamko la elimu bure wananchi wamekuwa wagumu sana kutoa michango mbalimbali ya kuboresha elimu.
Je, Serikali ina mikakati gani ya kumaliza tatizo la upungufu wa vyumba vya madarasa na vyumba vya maabara katika shule za msingi na sekondari?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vedastus Mathayo Manyinyi, Mbunge wa Musoma Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango wa Elimu Msingi bila Malipo unazingatia uendeshaji wa shule bila ada na michango kutoka kwa wazazi au walezi. Hata hivyo, mpango huo haujaondoa dhamira na uzalendo wa jamii kuchangia shughuli za maendeleo ya nchi yao kwa hiari. Kwa uzalendo wa wananchi walioonesha hivi karibuni Serikali imefanikiwa kupiga hatua za maendeleo katika sekta mbalimbali. Mfano, katika kufanikisha utengenezaji wa madawati kwa asilimia 97.2 kwa shule za msingi na asilimia 100.3 kwa shule za sekondari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatoa rai kwa wananchi wote ambao wamekuwa wagumu katika kushiriki shughuli za maendeleo wabadilishe mwenendo wao na kuwa na uzalendo kwa maslahi mapana ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mkakati wa kupunguza tatizo la nyumba, vyumba vya madarasa na maabara, Serikali katika bajeti ya mwaka 2016/2017 imetenga shilingi bilioni 29.3 kwa ajili yya ujenzi wa vyumba vya madarasa 3,306 kwa shule za msingi na shilingi bilioni 16.3 zimetengwa kujenga vyumba vya madarasa 1,047 kwa shule za sekondari. Aidha, kupitia MMES II zimetengwa shilingi bilioni 23.6 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa vyumba 1,642. Kwa upande wa maabara Serikali imetenga shilingi bilioni 18.9 kwa ajili ya ukamilishaji wa vyumba 2,135 vya maabara. Serikali itaendelea kutenga bajeti kila mwaka wa fedha na kuwashirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo katika kufanikisha upatikanaji wa elimu bora hapa nchini.