Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 3 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 35 2017-02-02

Name

Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Matumizi yasiyo sahihi ya lugha ya Kiswahili kwenye vyombo vya habari hayatoi fursa ya kukua kwa lugha yetu na badala yake yanachangia kurithisha lugha yetu kwa watoto kwa namna iliyo mbovu; mathalani, Mtangazaji wa runiga au redio anasema “hichi” badala ya “hiki” au nyimbo hii badala ya “wimbo huu” na kadhalika.
Je, Serikali ina mpango gani wa kimkakati wa kuvifanya vyombo vya habari kuwa mawakala wa kulinda usahihi wa lugha ya Kiswahili badala ya kuwa miongoni mwa wabomoaji wa lugha yetu?

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inaendelea kusimamia na kuratibu matumizi ya Kiswahili fasaha kwa vyombo vya habari. Hivi sasa inaandaliwa Sera ya Lugha ambayo itabainisha majukumu ya vyombo vya habari katika matumizi na uendelezaji wa lugha ya Kiswahili. Aidha, kwa sasa hatua mbalimbali zinachukuliwa katika kuhakikisha kuwa vyombo vya habari vinakuwa mawakala wa kulinda lugha ya Kiswahili, ambapo Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) kwa kushirikiana na wadau wa Kiswahili limeendelea kuendesha semina, warsha, makongamano na kutoa elimu inayohusu matumizi fasaha ya Kiswahili kwa waandishi wa vyombo vya habari mbalimbali pamoja na kuandika makala na vijitabu maalum na kuvisambaza kwa wanahabari kuhusu matumizi sahihi ya lugha ya Kiswahili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa lugha ya Kiswahili ni utambulisho na utamaduni wa Taifa letu na vile vile ndiyo lugha ya Taifa, waandishi wa habari wanalo jukumu kubwa la kuhakikisha lugha hii inaendelezwa ipasavyo, ikiwa ni pamoja na kuzingatia matumizi sahihi.
Aidha, mifano iliyotolewa na Mheshimiwa Mbunge ya “wimbo huu” na “hiki” ni mada za nomino na sarufi ambazo hufundishwa katika somo la Kiswahili katika shule za msingi na upili. Hivyo, napenda kutoa wito kwa wanafunzi ambao miongoni mwao ni wanahabari watarajiwa kujifunza masomo yote kwa bidii ikiwa ni pamoja na Kiswahili.
Vilevile wamiliki wa vyombo vya habari wazingatie ufaulu wa somo la Kiswahili kama moja ya sifa kwa waombaji wa kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwashauri wanahabari kutumia zana kama vile kamusi na vitabu vya miongozo ya uandishi na kuhudhuria makongamano ya Kitaifa na ya Kimataifa ya lugha ya Kiswahili, kwa mfano, Chama cha Kiswahili Afrika Mashariki (CHAKAMA) na Chama cha Wanafunzi wa Kiswahili Afrika Mashariki (CHAWAKAMA) ambayo hufanyika mwezi Septemba kila mwaka. Katika makongamano hayo, masuala ya kisarufi na ya kifasihi huwasilishwa na kujadiliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii itawasaidia kuongeza ujuzi na weledi wa lugha ya Kiswahili, kujua pia istilahi za kisayansi na kiteknolojia na hivyo kuandika na kutangaza kazi bora na zenye maudhui lengwa kwa jamii na kuepuka upotoshaji wa maneno ya Kiswahili usio wa lazima.