Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 1 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 12 2017-01-31

Name

Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Primary Question

MHE. DANIEL E. MTUKA aliuliza:-
Watanzania wengi wanahitaji umeme mjini na vijijini lakini wanashindwa kuvuta umeme kutokana na gharama kubwa ambapo service line ni shilingi 177,000 na zaidi na gharama ya nguzo ni shilingi 337,740 na zaidi:-
(a) Kwa kuwa nguzo ni mali ya TANESCO, je, kwa nini nguzo hizi zisilipiwe na Serikali?
(b) Je, Serikali haioni kuwa sasa ni wakati muafaka wa kupunguza service line costs kuwa shilingi 27,000 kama ilivyo kwa mradi wa REA?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Edward Mtuka, Mbunge wa Manyoni Mashariki, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, TANESCO hugharamia miundombinu ya umeme ikiwemo nguzo na vifaa vingine ili kupeleka umeme kwa wateja. Hata hivyo, kutokana na ufinyu wa bajeti si rahisi kupeleka miundombinu ya umeme maeneo yote kwa wakati mmoja. Kwa maeneo ambayo hayajafikiwa na miundombinu ya umeme wananchi kwa hiari ya kuchangia gharama husogeza miundombinu hiyo katika maeneo ili kuharakisha huduma hiyo. Aidha, kulingana na Kanuni za Sheria ya Umeme ya mwaka 2011, wateja wanaruhusiwa kugharamia miundombinu hiyo kisha kukubaliana na TANESCO namna ya kurejeshewa malipo hayo.
Mheshimiwa Spika, kwa maeneo ambayo tayari yamefikiwa na huduma ya umeme, wananchi huchangia kwa kulipia vifaa muhimu ikiwemo nguzo, mita pamoja na gharama nyingine.
Mheshimiwa Spika, Serikali inagharamia Miradi ya Umeme Vijijini (REA) kwa asilimia 100 na kiasi cha shilingi 27,000 wanacholipa wananchi ili kuunganishiwa umeme katika miradi hii ni kwa ajili ya gharama ya VAT tu. Lengo ni kuhamasisha na kuwawezesha wananchi wa vijijini ili wapate huduma hiyo kwa gharama nafuu. Baada ya miradi ya REA kukamilika, wateja huunganishiwa umeme kwa kufuata taratibu za TANESCO ambapo gharama yake ni shilingi 177,000 kwa umbali usiohitaji nguzo.
Mheshimiwa Spika, gharama za kuunganisha umeme kwa wateja wa majumbani maeneo ya mijini ni shilingi 320,960 kwa umbali usiohitaji nguzo ambapo wateja hufungiwa waya na mita. Gharama za maombi ya services charge ziliondolewa tangu tarehe 01 Aprili, 2016 lengo likiwa ni kupunguza gharama kwa wateja.