Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 1 Education, Science,Technology and Vocational Training, Ofisi ya Rais TAMISEMI. 2 2017-01-31

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JULIANA D. SHONZA Aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha miundombinu ya elimu vijijini kama nyumba za walimu pamoja na kulipa malimbikizo ya madeni ya walimu wanayoidai Serikali?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA Alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inaboresha miundombinu ya shule nchini kupitia mipango na bajeti ya Serikali kwa kushirikisha nguvu za wananchi na wadau wa maendeleo ili kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia.
Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali imetenga shilingi bilioni 13.9 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu 1,157 kwa shule za msingi na shilingi bilioni 11.14 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu 661 kwa shule za sekondari. Aidha, kupitia Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES II), Serikali imekamilisha ujenzi wa nyumba 146 kati ya nyumba 183 ambazo kila nyumba wataishi watumishi sita (walimu). Ujenzi wa nyumba hizo umegharimu shilingi bilioni 21.9. Nyumba 37 zinaendelea kujengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 5.5 na zitakamilika tarehe 30 Aprili, 2017.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kulipa madeni ya walimu kadri yanavyojitokeza na kuhakikiwa. Katika mwezi Oktoba, 2015 Serikali ililipa madeni ya shilingi bilioni 20.12 kwa walimu 44,700 na shilingi bilioni 1.107 zililipwa mwezi Februari, 2016 kwa walimu 3,221. Hivi sasa walimu wanadai Serikali madeni yanayofikia shilingi bilioni 26.04 kwa ajili ya walimu waliopo kazini 33,620 na walimu wastaafu 2,134. Deni hilo limewasilishwa Hazina kwa ajili ya taratibu za mwisho za kulipwa kwa walimu wanaodai.