Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 9 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 100 2016-11-10

Name

Yussuf Salim Hussein

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Chambani

Primary Question

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN aliuliza:-
Karibu theluthi moja ya ardhi ya Tanzania ni misitu na kuna uhaba mkubwa wa watalaam wa misitu nchini.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kukiboresha Chuo cha Misitu cha Olmotonyi?
(b)Je, kila mtalaam wa misitu aliyepo leo anasimamia hekta ngapi za eneo?

Name

Prof. Jumanne Abdallah Maghembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwanga

Answer

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Salim Hussein, Mbunge wa Chambani, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba kuna upungufu wa watalaam wa misitu nchini. Kwa sasa kila mtalaam wa misitu aliyepo anasimamia jumla ya hekta 25,000 za misitu. Kimsingi uwiano huu ni mara tano zaidi ya uwiano unaokubalika Kimataifa wa mtaalam mmoja kwa hekta 5, 000. Kwa kutambua hali hii, Wizara yangu imeanza kutatua tatizo hili kwa kuboresha miundombinu ya Chuo cha Misitu Olmotonyi.
Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushirikiana na Serikali ya Norway inatekeleza mradi wa kuwezesha jamii kupitia mafunzo ya shughuli za usimamizi shirikishi wa mistu na mabadiliko ya tabianchi. Mradi huu unalenga kukijengea chuo uwezo kwa kukarabati nyumba za watumishi saba, kuimarisha maktaba ya chuo kwa kuweka samani, vitabu vya kiada na vitabu 137 vya mada 22 tofauti, vifaa 62 vya kufundishia, kompyuta 15 na kutoa mafunzo ya kompyuta kwa wakutubi watano; ukarabati wa mtandao wa mawasiliano na kuunganisha chuo na Mkongo wa Taifa.
Mheshimiwa Spika, pia mradi unaendelea na ujenzi wa bweni moja lenye uwezo wa kuchukua wanachuo 100 na ukumbi wa mihadhara wenye uwezo wa kuchukua wanachuo 200 kwa wakati mmoja. Vilevile mradi umewajengea uwezo wa kutumia mbinu bora za kufundisha wahadhiri 16 wa chuo hicho. Mradi unatoa mafunzo kwa jamii ya vijijini kuhusu kuhifadhi misitu na shughuli mbadala za kiuchumi.
Mheshimiwa Spika, kupitia mradi huu, Serikali inatoa ufadhili kwa wananfunzi wa ngazi za cheti na ngazi za diploma ili waweze kukamilisha mafunzo yao katika chuo chetu.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miaka mitatu, kuanzia mwaka 2013/2014 mpaka 2015/2016, Wizara kupitia Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania imegharamia ukarabati wa nyumba tisa za watumishi, kumbi za chakula na mikutano; na ununuzi wa kompyuta mbili na basi aina ya Tata kwa ajili ya usafiri wa wanafunzi wanapokwenda kupata mafunzo nje ya chuo.
Mheshimiwa Spika, kutokana na hatua hizi, chuo kumeongeza uwezo wake wa kupokea wanafunzi wengi zaidi na kuwajengea uwezo wawe wataalamu mahiri katika ngazi ya masomo yao.